NAIBU Spika wa Bunge la Tanzania, Dk. Tulia Ackson amejitosa kuwania nafasi ya juu ya uongozi wa Bunge kwa kuchukua fomu ya kuwania uspika. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Dk. Tulia amekabidhiwa fomu hizo leo Jumatatu, tarehe 10 Januari 2022 na Katibu msaidizi Mkuu Idara ya Organaizesheni, Solomon Itunda katika Ofisi za Makao makuu ya CCM Dodoma.
Dk. Tulia anaungana na wanachama wengine wa CCM akiwemo, Mbunge wa Mlimba, Godwin Kunambi na mbunge wa zamani wa Shinyanga Mjini, Stephen Masele ambao nao wamechukua fomu.
“Nimeomba nafasi ya kuwa spika ili niweze kuliendesha Bunge kwa misingi ya kanuni, sheria na taratibu na kuhakikisha muhimili wa Bunge unasimamia sheria na kulifanya Bunge kufanya kazi kwa karibu na serikali,” amesema Dk. Tulia
Kuhusu nafasi yake ya sasa, Dk. Tulia amesema, katiba inataja watu ambao hawastahili kugombea kuwa ni waziri mkuu na mawaziri lakini yeye sheria hamzuii kugombea, “na bado nafasi yangu ya unaibu spika baijawa wazi.”
CCM inaendesha mchakato wa ndani wa kumpata mgombea mmoja wa kwenye kuwania uspika baada ya aliyekuwa Spika Job Ndugai kutangaza kujizulu nafasi hiyo tarehe 6 Januari 2022.
Alichukua uamuzi huo baada ya kauli yake kuhusu mikopo inayokopwa na serikali kupokelewa kwa mtazamo tofauti na wana CCM akiwemo Rais Samia Suluhu Hassan aliyesema, hakuna nchi isiyokopa.
Leave a comment