MBUNGE Viti Maalum, Grace Tendega, amedai Katibu Mkuu wa Chama cha Chadema, John Mnyika, alishiriki kikao cha Sekretarieti ya Baraza la Wanawake la chama hicho (BAWACHA), kilichoitishwa kwa ajili ya kuteua majina ya wabunge viti maalum. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Tendega ametoa madai hayo leo Alhamisi, tarehe 13 Oktoba 2022, katika Mahakama Kuu, Masjala Kuu, jijini Dar es Salaam, mbele ya Jaji Cyprian Mkeha, wakati wa usikilizwaji wa kesi aliyofungua yeye na wabunge wenzake viti maalum 18, kupinga kufukuzwa Chadema.
Ni baada ya Wakili wake, Ipilinga Panya kumuuliza maswali ya ufafanuzi, kuhusiana na maswali ya dodoso aliyoulizwa na Wakili wa mjibu maombi wa kwanza-Bodi ya Wadhamini ya Chadema, Peter Kibatala, ambaye alimuonyesha taarifa kuhusu kikao Cha Kamati Kuu ya Chadema, kilichofanyika tarehe 7 Novemba 2020.
Wakili Panya alimhoji Tendega kuwa, anaiambia nini mahakama hiyo kuhusu tarehe hiyo ambapo alijibu akidai siku hiyo alikuwa na kikao cha Sekretarieti ya Bawacha na kwamba yeye alikuwa mwenyekiti wa kikao hicho kilichokuwa kinaandaa majina ya wabunge viti maalum.
Amedai, katika kikao hicho Mnyika alikuja akiwa na majina 10 kutoka Baraza la Vijana la Chadema (BAVICHA) likiwemo la aliyekuwa Katibu Mkuu wake, Nusrat Hanje na kuagiza lisiachwe kwenye uteuzi huo kwani alikuwa Yuko mahabusu.
“Tulifanya kikao Cha BAWACHA lakini Mnyika alikuja wakati tunaandaa majina ya wagombea ubunge viti maalum… Katibu mkuu alikuja na majina 10 ya BAVICHA ambayo alisisitiza jina la Nustat Hanje tusiliache sababu yeye yuko mahabhsu. Hicho kikao ndicho nilishiriki,” amedai Tendega.
Wakati Tendega anaendelea kuulizwa maswali hayo, aliiomba mahakama icheze video ya Mnyika, aliyokuwa anazungumzia sakata lao alidai kwamba alitoa kauli iliyotoa hukumu dhidi Yao kabla ya vikao husika kuketi.
Katika video hiyo, Mnyika alinukuliwa akisema Chadema hakikufanya uteuzi huo na wala hakikupeleka majina hayo katika Time ya Taufa ya Uchaguzi (NEC), Kwa ajili ya uteuzi huku akidai uteuzi huo ulifanywa na mfumo wa Serikali.
Kupitia video hiyi, Mnyika alinukuliwa akihoji Kwa ninj Hanje aliapishwa muda mfupi baada ya kutokewa mahabusu jijini Dodoma, kabla ya mahakana haijatoa uamuzi dhidi ya mashtaka yaliyokuwa yanamkabili.
Tendega anaendelea kuulizwa maswali ya ufafanuzi na Wakili Panya. Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online.
Leave a comment