KESI namba 36/2022 ya kupinga kuvuliwa uanachama wa Chama Cha Chadema, iliyofunguliwa na wabunge viti maalum 19 wakiongozwa na Halima Mdee, inaendelea kusikilizwa katika Mahakana Kuu, Masjala Kuu, jijini Dar es Salaam. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kesi hiyo inasikilizwa Leo Alhamisi, tarehe 13 Oktoba 2022, mahakamani halo mbele ya Jaji Cyprian Mkeha, ambapo Mbunge Viti Maalum, Grace Tendega, anamalizia kuulizwa maswali ya ufafanuzi kuhusu malalamiko aliyoyaweka kwenye hati yake ya kiapo.
Tendega alianza kuulizwa maswali ya dodoso na upande wa mjibu maombi wa kwanza katika kesi hiyo, Bodi ya Wadhamini Chadema, Ijumaa iliyopota.
Tendega aliulizwa maswali hayo na Wakili Peter Kibatala, ambapo alihojiwa alisaini wapi hati hiyo na kujibu aliisaini tarehe 18 Julai 2022, jijini Dar es Salaam.
Pia, Tendega alihojiwa na Kibatala kuhusu flash zilizokuwa na video zinazoonesha Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika na Mwenyekiti wa Chama hicho, Freeman Mbowe, wakizungumzia sakata lao, kupitia mkutano wao na vyombo vya habari.
Tendega alijibu swali Hilo akidai, flash zenye video zilizokuwa na hotuba za viongozi hao, zimewekwa katika hati yake ya kiapo kama ushahidi kuwa mchakato uliotumika kuwavua uanachama haukuwa halali kwani Mnyika na Mbowe walitoa kauli zilizotoa uamuzi kabla vyombo vya maamuzi kutoa maamuzi.
Katika video hizo, Mnyika alinukuliwa akisema Chadema haikuteua majina ya wabunge viti maalum kwenda bungeni, hivyo kilichofanywa na Mdee na wenzake ni usaliti Kwa chama hicho na kutoa wito kwa wanachama kutoa maoni Yao juu ya hatua zinazopaswa kuchukuliwa dhidi Yao.
Naye Mbowe alinukuliwa akisema Chadema Haina wabunge bungeni na kwamba haiwatambui.
Leo, Tendega anaulizwa maswali ya ufafanuzi na Wakili wake, Ipilinga Panya, Kisha akimaliza anaanza kuhojiwa mbunge mwingine, Hawa Mwaifunga.
Mdee na wenzake walifungua kesi hiyo baada ya Baraza Kuu la Chadema, kutupilia mbali rufaa zao za kupinga kufukuzwa Chadema, Kwa tuhuma za usaliti.
Mdee na wenzake, wanaiomba mahakama ifanye mapitio ya kimahakama juu ya mchakato uliotumika kuwafukuza ndani ya Chaka hicho, wakidai ulikuwa kinyume Cha Sheria Kwa kuwa hawakupewa haki ya kusikilizwa na ulikuwa wa upendeleo.
Leave a comment