SELEMANI Maziku, amepandishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, kwa tuhuma za kujipatia Sh. 140 milioni, baada ya kughushi ridhaa ya mke wake, Scora Bundala. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Maziku amepandishwa kizimbani hapo leo Alhamisi, tarehe 15 Desemba 2022, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Mary Mrio, na kusomewa mashtaka yanayomkabili na Wakili wa Serikali, Yusuph Aboud.
Wakili Aboud, amedai kuwa, Maziku ambaye ni mkazi wa Kitunda Mwanagati jijini Dar es Salaam, mnamo tarehe 10 Desemba 2022, katika mahali kusikojulikana alighushi ridhaa ya mkewe, na kuiwasilisha katika Benki ya Stanbic kisha kujipatia mkopo wa Sh. 140 milioni, bila ya ridhaa ya mke wake.
Mbele ya Hakimu Mrio, Maziku alikana kutenda kosa hilo, huku upande wa mashtaka ukiieleza mahakama hiyo kuwa upelelezi wa mashtaka yanayomkabili umekamilika.
Mshtakiwa huyo amrudishwa rumande hadi tarehe 28 Desemba 2022, baada ya kushindwa kukamilisha masharti ya dhamana ya kuleta wadhamini wawili watakaotoa pesa Sh. 70 milioni kila mmooja au kuwasilisha hati ya mali isiyohamishika yenye thamani hiyo.
Leave a comment