IDARA ya Uhamiaji nchini Tanzania, imewataka Watanzania kuwa makini dhidi ya vitendo vya utapeli vilivyoibua katika mchakato wa maombi ya nafasi za ajira 500 ilizotangaza hivi karibuni. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Tahadhari hiyo imetolewa jana tarehe 14 Desemba 2022 na Msemaji Mkuu wa Idara ya Uhamiaji, Paul Mselle, akisema tangu nafasi hizo zitangazwe kumekuwepo na taarifa zenye lengo la kuwalaghai wananchi kupitia mitandao ya kijamii na baadhi kupigiwa simu na wanaotaka fedha ili wawasaidie kupata ajira hizo.
Taarifa ya Mselle imeeleza kuwa, hakuna malipo yoyote yanayohitajika kwa ajili ya waombaji kupata nafasi za ajira, hivyo wananchi wapuuze wanaowaomba fedha huku wakitakiwa kutoa taarifa kwa vyombo vya ulinzi na usalama pindi wanapopokea ujumbe unaowataka kutuma fedha ili waweze kupatiwa nafasi hizo.
“Idara inapenda kuufahamisha umma kuwa, mchakato wa ajira unaendeshwa na kusimamiwa kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za ajira kama ilivyoanishwa kwenye tangazo la ajira,” imesema taarifa ya Mselle.
Nafasi hizo za ajira zilitangazwa tarehe 11 Desemba 2022 na Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dk. Anna Makakala, kwa vijana wa Kitanzania waliohitimu mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) au Jeshi la Kujenga Uchumi (JKU).
Leave a comment