WANANCHI wa Kisiwa cha Rukuba, kilichopo Jimbo la Musoma Vijijini, mkoani Mara, wameamua kuanza ujenzi wa shule ya sekondari kwa nguvu zao, ili kuondoa mateso wanayopitia watoto wao kwenda umbali mrefu kufuata shule. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mara…(endelea).
Ujenzi huo ulioanza tangu Oktoba na unaendelea hadi sasa, ambapo Mbunge wa Musoma Vijijini, Prof. Sospeter Muhongo (CCM), ametoa mifuko ya saruji 150 kwa ajili ya kufanikisha utekelezaji wake.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na ofisi ya Mbunge wa Musoma Vijijini, jana tarehe 1 Novemba 2023, wananchi hao wameanza ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa na ofisi moja ya walimu, huku wakitegemea wadau mbalimbali pamoja na Serikali, watawaunga mkono ili shule ipatikane.
“Wakazi wa Kisiwa cha Rukuba wameamua kujenga sekondari yao ili elimu ya sekondari itolewe hapo Kisiwani badala ya wanafunzi kwenda kupanga vyumba nchi kavu (Kijijini Etaro) kwa ajili ya elimu yao ya sekondari,”
“Harambee ya kwanza ya ujenzi wa Sekondari ya Kisiwa cha Rukuba ilishafanyika chini ya usimamizi wa Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini, akishirikiana na Kamati ya Siasa ya Wilaya ya Musoma Vijijini,” imesema taarifa hiyo.
Prof. Muhongo amewataka wadau mbalimbali kuwaunga mkono wananchi wa Rukuba, ili wamalize ujenzi wa shule yao.
Hadi sasa shule tano za sekondari zinajengwa na wananchi wa Musoma Vijijini, ili kuboresha mazingira ya utoaji elimu jimboni humo.
Leave a comment