CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimeungana na kauli ya serikali kwamba ‘hakuna kuweka mpira kwapani.’ Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Kauli hiyo, ilianza kutumiwa na Selemani Jafo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), na sasa imebebwa na CCM.
“Hakuna kuweka mpira kwapani…, tunaishukuru serikali kwa kuwa na msimamo,” amesema Humphrey Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM wakati akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 13 Novemba 2019, jijini Dar es Salaam.
Polepole amesema, vyama vya upinzani vimeamua kujitoa baada ya kuonea dalili za kushindwa katika uchaguzi huo.
Siku tatu zilizopita, Waziri Jafo akizungumza na wanahabari jijini Dodoma alisema, ‘hakuna kuweka mpira kwapa,’ alikuwa akizungumzia hatua ya vyama vya upinzani kujiondoa kwenye uchaguzi huo.
“Nimesema hakuna kuweka mpira kwapani, hakuna kukimbia. Hapa mpaka kieleweke…,” alisema Jafo.
Hata hivyo, vyama vilivyojitoa – Chadema, ACT-Wazalendo, CUF, UPDP, NCCR-Mageuzi na Chaumma – vimeendelea kuwa na msimamo wa kutoshiriki uchaguzi huo.
CCM nayo imeendelea kukazia kauli hiyo na kuongeza, kwamba vyama vya upinzani vimejitoa kutokana na ‘kushindwa’ mapema.
Polepole amedai, vyama vya upinzani vinajua havikubaliki kwa wananchi, huku akidai CCM kukubalikwa kutokana na maendeleo yaliyofanywa na serikali iliyo chini yake.
“Wapinzani ni waungwana, wakasema mambo yatakayotokea kwenye chama chetu, wakaona uchaguzi 2014 ulikuwa Tsunami, wa mwaka huu ni wa Kisulisuli, wakaona bora kuweka mpira kwapani,” amesema Polepole.
Aidha, Polepole ameitaka serikali kuwa na msimamo kwa kutosikiliza mapendekezo ya upinzani, ya kuaghirisha uchaguzi huo, ili dosari zilizojitokeza zipatiwe mwarobaini.
Amedai, mchakato wa uchaguzi unaendeshwa kwa haki, na kuwa kama kuna mtu ana malalamiko, afuate taratibu za kukata rufaa.
“Tulitaka serikali isimame kwenye jambo hili, isiyumbe kwenye jambo hili sababu ni jambo la kisheria na kanuni, na wote tulishiriki kukubaliana mtu akikosea kwenye sheria, sheria ni msumeno hukata kote. Ukikosea kwa ujinga wako, sheria haina huruma,” amesema Polepole.
Hata hivyo, Polepole ameshindwa kueleza malalamiko ya upinzani kutokana na wasimamizi wa uchaguzi baadhi ya maeneo kutofungua kabisa ofisi zao, kugoma kupokea fomu, kugoma kupokea rufaa, kupigwa na kunyang’anywa fomu zao.
Leave a comment