SELEMANI Jafo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), sasa anashinikizwa kujiuzulu. Anaripoti Martini Kamote…(endelea).
Imeelezwa, ni kwa madai ya kushindwa kusimamia uchaguzi wa serikali za mitaa, na kusababisha vyama vya upinzani kuutelekeza kutokana na kuvurugwa na wasimamizi wake.
Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 13 Novemba 2019, Chiku Abwao ambaye ni Mwenyekiti wa Wanawake wa Chama cha ACT-Wazalendo – Taifa amedai, Waziri Jafo anahusika katika kuvuruga uchaguzi.
“Inampasa ajiuzulu, ameshindwa kusimamia uchaguzi, ameamua kupuuza malalamiko ya vyama vyetu na kukibeba chama chake –CCM- kwa kuumiza vyama vyetu.
“Amekuwa akitoa kauli zenye kupingana, huo ni ushahidi tosha kwamba ameshindwa kazi, ili uchaguzi ufanyike kunahitajika usawa ambao chini ya uongozi wake, umeshindwa kupatikana, lakini cha ajabu amekubali kutumika,” amesema.
Amesema, kama uchaguzi huo utafanyika, Wanawake wa ACT-Wazalendo hawatawatambua na wala kutoa ushirikiano kwa viongozi watakaochaguliwa.
“Huu ni uchaguzi wa chama kimoja katika serikali inayojitangaza kuwa na mfumo wa vyama vingi, kati serikali haiwezi kujinasibu kwa kusimamia uchafu huu na kuubariki,” Abwao amemweleza mwandishi wa habari hii.
Amesema, uzoefu unaonyesha kuwa migogoro mingi, hasa ya kutumia nguvu huaathiri zaidi wanawake na watoto kuliko makundi mengine ya jamii.
“Tunawaomba viongozi wetu wa chama kukutana na vyama vyote makini vya siasa, ili kuwa na msimamo wa pamoja katika hili la kufutwa uchaguzi huu,” amesema.
Leave a comment