NAIBU Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Sisty Nyahoza, amevitaka vyama vya siasa kurekebisha dosari za ndani zinazoleta changamoto katika chaguzi, badala ya kukimbilia kudai marekebisho ya katiba. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Nyahoza ametoa kauli hiyo leo tarehe 23 Agosti 2023, jijini Dar es Salaam, katika mkutano wa taifa wa kujadili hali ya demokrasia nchini kuelekea Uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa 2024 na Uchaguzi Mkuu wa 2025.
“Tusifikiri uchaguzi ni lazima kukimbilia kwenye katiba, uchaguzi ni kujirekebisha sisi wenyewe ndani ya vyama na watendaji wa uchaguzi wawe professional , waweke uwazi. Hata uwe na katiba nzuri kiasi gano kama kwenye uchaguzi huna maadili hiyo katiba nzuri haikusaidii,” amesema Nyahoza.
Nyahoza ametaja changamoto zilizoko ndani ya vyama vya siasa ambazo zinasababisha malalamiko katika uchaguzi, ikiwemo uteuzi wa wagombea wanaopenda rushwa na uteuzi wa watendaji wa uchaguzi wasiokuwa na maadili.
“Changamoto ya rushwa inalalamikiwa katika uchaguzi inafanya kuwe na matatizo katika kuwa na uchaguzi huru na haki. Changamoto hizi zipo sehemu mbili, katika uchaguzi wa kushindana chama na chama na zipo katika uteuzi ndani ya vyama. Usipotibu kule na usipokuwa na malezi mazuri ndani ya vyama hauwezi kuwa na uchaguzi mzuri,” amesema Nyahoza.
Nyahoza amesisitiza “wagombea mnaohisi wanatoa rushwa mkiwakata ndani ya vyama vyenu, na wale mnaohisi wataleta shida kule kwenye uchaguzi hawataheshimu sheria mkiwatoa huko, badi uchaguzi baina ya vyama utakuwa mzuri na tunaamini matatizo mengi yataisha na kama sheria zitarekebishwa.”
Mlezi huyo wa vyama vya siasa, amevitaka kuwafundisha wanachama wake misingi ya demokrasia katika chaguzi, ikiwemo kukubali matokeo ya kushinda na kushindwa.
Nyahoza ametoa ushauri huo baada ya baadhi ya washiriki kuitaka Serikali ikamilishe mchakato wa marekebisho ya sheria za uchaguzi na katiba, ili chaguzi zijazo ziwe huru na haki.
Leave a comment