MAKAMU wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Othman Masoud Othman, amewataka wananchi visiwani humo, kudumisha umoja na mshikamano ambao ndiyo njia kuu ya kuisadia Zanzibar kusonga mbele zaidi kimaendeleo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Othman ameyasema hayo jana mara baada ya swala ya Ijumaa tarehe 5 Machi 2021, katika Msikiti wa Masjid Arafa uliopo Mombasa Wilaya ya Magharib ‘B’ Mkoa wa Mjini Magharib Unguja.
“Rangi za vyama vyetu wala itikadi za vyama vyetu vya siasa, kwa sasa sio suluhisho la ukombozi wa Zanzibar na badala yake tuwe wamoja na kuhakikisha tunajenga mapenzi na nchi yetu ili kuleta maendeleo, kwani maendeleo yakija kila mwananchi atafaidika bila kuangalia itikadi yake,” alisema Othuman
Ni kwa mara ya kwanza kwa Othuaman kuswali swala ya Ijumaa akiwa makamu wa kwanza wa rais, baada ya kuapishwa tarehe 3 Machi 2021, na Rais wa Zanzibar, Hussein Mwinyi, ambaye siku moja kabla alimteua, baada ya jina lake, kuwasilishwa na ACT-Wazalendo.
Othuman, aliapishwa kushika wadhifa huo, baada ya kufariki dunia kwa Maalim Seif Sharif Hamad, tarehe 17 Februari 2021, katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Dar es Salaamn alipokuwa amelazwa.
Akisisitiza hilo, Othman alisema, “mimi jukumu langu kubwa ni kumsaidia Rais kutimiza ndoto ya maendeleo ambayo italetwa na umoja na mshikamano wa viongozi na wananchi kwa pamoja.”
“Tukifanya hili, itakuwa ni dua kubwa pia kwa kiongozi wetu Maalim Seif kwani hili aliliasisi na kulisimamia,” alisema
Othman alisema ni wazi katika kupigania hili na kufikia maendeleo kuna changamoto nyingi lakini, wananchi wakiwa wamoja na mshikamano basi nguvu itakuwa kubwa na mafanikio yatapatikana.
Makamu huyo wa kwanza wa Zanzibar aliyewahi kuwa mwanahseria mkuu visiwani humo aliwataka waumini hao kujua ili kiongozi afanye kazi zake na mambo kwenda vizuri basi ni lazima wananchi wawe tayari na wawe wema kama wema wanaoutafuta kwa kiongozi wao.
Leave a comment