MBUNGE Viti Maalumu, Stella Ikupa, ametishia kushika shilingi katika makadirio ya bajeti ya Wizara Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwa mwaka wa fedha wa 2022/23, endapo waziri wake, Innocent Bashungwa, hatoa maelezo ya kina juu ya halmashauri kutotoa mafuta ya watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Ikupa ametoa msimamo huo leo Jumanne, tarehe 19 Aprili 2022, akichangia mjadala kuhusu makadirio ya bajeti hiyo, bungeni jijini Dodoma.
“Nimuombe waziri anapokuja kuhitimisha basi aweze kuelezea suala hili kwa kina, kwa nini halitekelezeki lakini pia niseme wazi maelezo ya waziri yasiponitosheleza nitashika shilingi yake, nitaondoka na huo mshahara wake,” amesema Ikupa.
Ikupa amesema halmashauri nyingi zimekuwa zikikiuka kanuni na miongozo inayoziagiza kutoa mafuta hayo kwa maalbino.
“Changamoto ya utolewaji mafuta ya watu wenye ualbino kwenye halmshauri zetu imekuwa ya muda mrefu, miongozo ipo, kanuni zinaongea wazi lakini suala hili halitekelezeki kwenye halmashari zetu, nimekuwa nikipokea simu kutoka kwa watu wenye ulemavu wakilalamikia suala hili, kwamba halmashauri hazito mafuta,” amesema Ikupa.
Ikupa amesema “Niiombe Serikali suala hili liweze kutekelezwa kwa maana ya kwamba halmashauri ziweze kutenga kununua na kusambaza mafuta haya kwa watu wenye ualbino.”
Katika hatua nyingine, Ikupa ameishauri Serikali iweke utaratibu maalumu utakaowezesha watu wenye ulemavu kupata huduma za afya bure, kama ilivyofanya kwa wazee wasiokuwa na uwezo.
“Lakini sambamba na hilo, niweke wazi watu wenye ulemavu walio wengi wanaishi kwenye kipato cha chini sana, kwa maana kwamba inapelekea kushindwa kumudu matibabu yao,” amesema Ikupa na kuongeza;
“ Niombe Serikali iweze kufanya zoezi lililofanyika kwa wazee, kuwatambua na kuwapatia vitambulisho wale ambao hawana uwezo wa kupata matibabu, ili basi vitambulisho vile viwawezeshe kutibiwa kwa urahisi.”
Leave a comment