MBUNGE Viti Maalumu, Sophia Mwakagenda, ameishauri Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, itumie matokeo ya nyuma ya wanafunzi katika kuamua ufaulu wa mtihani wa mwisho wa kidato cha nne, ili kuwasaidia wanaochanganyikiwa wakati wakifanya mitihani hiyo ya kuhitimu elimu ya sekondari. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Mwakagenda ametoa ushauri huo leo Jumatano, tarehe 25 Mei 2022, katika kipindi cha maswali na majibu, bungeni jijini Dodoma.
“Hamuoni kwamba mtihani wa mwisho wa kidato cha nne mwanafunzi anapofanya wakati mwingine anaweza akawa amechanganyikiwa. Kwa nini wizara isiangalie matokeo ya nyuma jumlisha na yale ya mwisho tuweze kumhukumu kuendelea na maisha yake,” amesema Mwakagenda.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Omary Kipanga, amesema katika upangaji wa matokeo ya mtihani wa kidadto cha nne, huchukua asilimia 30 ya maendeleo yake ya elimu katika kipindi cha miaka minne, kisha inajumlisha asilimia 70 ya matokeo ya mtihani wa mwisho.
“Naomba nimhakikishie mbunge kwamba mtihani wetu wa mwisho ule wa form four sio unaopelekea kuwa na matokeo ya mwisho. Mtihani wetu una maeneo mawili, asilimia 30 inakuwa kwenye maendeleo ya elimu. Asilimia 30 zinatoka kwenye maendeleo yake aliyofanya miaka minne,” amesema Kipanga ana kuongeza:
“Asilimia 70 zinazingatiwa kwenye ule mtihani wake wa mwisho iwapo kama amefanya vizuri kwenye maendeleo yake kutoka kidato cha kwanza mpaka cha nne. Ile asilimia 30 itambeba na kuchangia asilimia 70 ya matokeo yake. Hilo Serikali limezingatia na ndilo linaendelea mpaka sasa.”
Leave a comment