KATIBU wa Idara ya Haki za Binadamu na Makundi Maalum wa ACT-Wazalendo Taifa, Mbarala Maharagande ametangaza vipaumbele vyake vinne aliyoahidi kuanza navyo kazi endapo atachaguliwa kushika nafasi ya Kiongozi wa chama hicho, inayoshikiliwa na Zitto Kabwe, aliyetangaza kung’atuka baada ya muda wake kuisha. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Maharagande ambaye pia ni Msemaji wa ACT-Wazalendo katika masuala ya katiba na sheria, ametangaza vipaumbele hivyo jana tarehe 23 Februari 2024.
Miongoni mwa vipaumbele alivyotaja Maharagande, ni kuweka mikakati itakayokipa ushindi ACT-Wazalendo kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa 2024 na uchaguzi Mkuu wa 2025. Pia, ameahidi kuanzisha mfuko wa kuwasaidia wanaokipigania chama hicho.
“Nikichaguliwa nini nitafanya? Kuimarisha umoja ndani ya chama, kuwatambua wapiganaji wa chama wazee kwa vijana walioshiriki kujenga chama. 2025 baada ya ushindi wa viti vya ubunge, uwakilishi na udiwani,” amesema Maharagande na kuongeza:
“Nitaanzisha mfuko wa kuwasaidia waliokipigania na wanaoendelea kukipigania chama utakaojulikana kama KC Fund, nitaweka utaratibu wa kukutana na kuwasikiliza viongozi, wanachama na wananchi kila mwezi mara moja.”
Katika uchaguzi huo unaotarajiwa kufanyika mwanzoni mwa Machi 2024, Maharagande atachuana vikali na Makamu Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo Bara, anayemaliza muda wake, Dorothy Semu.
Leave a comment