JESHI la Polisi kupitia chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es Salaam (DPA) kimeandaa mashindano ya Polisi Jamii yatakayoshirikisha wananchi pamoja na askari wa jeshi hilo lengo likiwa ni kuwaleta karibu wananchi na Jeshi la Polisi katika kutokomeza uhalifu na kuchangia damu katika benki ya damu salama. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza na vyombo vya habari chuoni hapo leo tarehe 15 Agosti, 2023, Mkuu wa Chuo hicho, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Dk. Lazaro Mambosasa, amesema lengo la mashindano hayo ni kuwashirikisha wananchi katika michezo ambayo itawakutanisha na askari wa Jeshi la Polisi ambapo watabadilishana taarifa mbalimbali zikiwemo za uhalifu na wahalifu katika maeneo yao.
Mbali na burudani itakayotolewa na michezo hiyo, pia jeshi hilo kupitia wakufunzi na wanafunzi wa chuo hicho pamoja na washiriki wengine kutoka nje wanakusudia kuchangia damu katika benki ya damu salama, zoezi ambalo linatarajiwa kusimamiwa na hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Temeke.
Kwa upande wake Afisa Michezo wa chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es salaam (DPA), Mratibu Mwandamizi wa Polisi SSP, Salum Madongo amesema katika mashindano hayo wanatarajia kuhusisha michezo 16 ikiwemo mpira wa miguu kwa wanaume na wanawake, mpira wa wavu, masumbwi, taekwondo, judo, riadha na mingine.
Naye Kocha wa mpira wa kikapu, Lincon Kagame, amesema wamefarijika kualikwa na kushiriki michezo ya Polisi Jamii ambapo amebainisha kuwa michezo hiyo itawaleta karibu na kuwaunganisha na jeshi la Polisi katika kupambana na uhalifu.
Mashindano hayo yanatarajiwa kuzinduliwa tarehe 25 Agosti 2023 ambapo itakuwa siku ya ugawaji wa vifaa mbalimbali kwa timu zote shiriki pamoja na zoezi la uchangiaji wa damu na huku michezo ikianza rasmi tarehe 4 Septemba na kumalizika tarehe 23 Septemba, 2023.
Leave a comment