MBUNGE wa Mchinga mkoani Lindi (CCM), Mama Salma Kikwete,ameiomba Serikali ipeleke maji safi na salama kwa wananchi wa jimbo hilo. Anaripoti Mwandishi Wetyu, Dodoma…(endelea).
Mama Salma ametoa ombi hilo leo Jumanne, tarehe 29 Juni 2021, katika kipindi cha maswali na majibu, bungeni jijini Dodoma.
Mke huyo wa Rais Mstaafu, Jakaya Kikwete, ameiomba Serikali ilifikirie jimbo lake, kwa kuwa linakabiliwa na uhaba wa maji safi na salama, huku akiishauri itoe maji katika chanzo cha Ng’apa, kisha iyasambaze jimboni humo.
“Maji ni uhai kwa viumbe vyote, ni muhimu kwa ustawi. Naomba kuuliza swali langu, jimbo langu la Mchinga halina maji safi na salama. Sasa ningeomba jimbo hili lifikiriwe kwa umakini mkubwa, kupata maji safi na salama kutoka chanzo kikubwa cha Ng’apa,” amesema Mama Salma na kuongeza:
“Je, ni lini maji safi na salama yatapelekwa Mchinga, kwa wananchi wa jimbo hio?”
Akijibu swali hilo, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema atafika katika jimbo hilo, ili aangalie namna ya kutatua changamoto zake za huduma ya maji.
“Najua changamoto za watu wake, siku zote anayelala na mgonjwa anajua mhemo wa ugonjwa. Naomba nimpe upendeleo maalumu, moja kufika kwanza katika jimbo lake,” amesema Aweso na kuongeza:
“Pili tunatambua tuna chanzo toshelevu cha Ng’apa, tumejenga mradi wa maji Lindi. Tunataka tuyatoe maji ya Ng’apa ili tuhakikishe yanafika Mchinga ili wananchi waondokane na matatizo ya maji.”
Leave a comment