HATIMAYE aliyekuwa Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ameteuliwa na Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi akichukua nafasi ya Sophia Mjema. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Pia halmashauri hiyo iliyokutana leo tarehe 22 Oktoba, 2023 mjini Dodoma, katika ikao chake maalum, chini ya Mwenyekiti Samia Suluhu Hassan, imeridhia kuielekeza Serikali kuendelea na hatua ya utiaji saini mikataba ya uendelezaji na uwekezaji wa bandari.
Katika taarifa iliyotolewa na Idara ya Itikadi na Uenezi CCM, Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, imefanya mabadiliko madogo ya Sekreterieti ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, kwa kumteua Makonda kuwa Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Itikadi na Uenezi.
Makonda amechukua nafasi ya Sophia Edward Mjema ambaye ameteuliwa kuwa Mshauri wa Rais Masuala ya Wanawake, Watoto na Makundi Maalum.
Pia Halmashauri Kuu ya CCM Taifa pia imemteua Rabia Abdallah Hamid kuwa Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI).
Rabia amechukua nafasi ya Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk ambaye ni Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Uhusiano wa Afrika Mashariki.
Leave a comment