RAIS Samia Suluhu Hassan ameagiza kuanzishwe kikosi kazi ambacho kitashughulikia nishati safi ya kupikia kitakachotoa mapendekezo pamoja na dira ya miaka 10 ya namna ya kuhamia kwenye nishati hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia ametoa maelekezo hay oleo tarehe mosi Novemba, 2022 katika Kongamano la Kitaifa la Nishati Safi ya Kupikia linalofanyika kwa siku Novemba 1-2, 2022 jijini Dar es Salaam.
Amesema kikosi kazi hicho ambacho kitaongozwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa chini ya uratibu wa wiara ya nishati na madini kitahusisha sekta zinazohusika na nishati, makamu wa rais, ofisi ya waziri mkuu sera ya uratibu, wizara ya madini, wizara maendeleo ya jamii na sekta binafsi
“Nataka mchambue sera za serikali tuone sekta binafsi wataingiaje na wanatoa mapendekezo gani katika sera zetu. Lakini pia wadau wa maendeleo nao washiriki kwa sababu ni watekelezaji wa sera hizi na wanafanya kazi moja kwa moja na taasisi nyingine.
“Kikosi kazi kitakuja na mpango mkakati ambao utatuelekeza kwenye utekelezaji na kutafuta suluhu ya nishati safi na endelevu ya kupikia.
“Ni lazima tuende na nishati safi kwa maendeleo ya nchi, kukinga haki za wanawake kwani wanatumika kuumiza afya zao bila malipo, wanasonga ugali huku machozi yanatoka, macho yameharibika… akina mama wa aina hii wapo wengi,” amesema Rais Samia.
Amesema nishati safi ya kupikia itawapunguzia mzigo akina mama pamoja na madhara wanayoyapata bila hata malipo.
“Ukimrahisishia mama kupata nishati safi ya kupikia, unampa muda zaidi wa kushughulikia na mambo yake ya kiuchumi,” amesema.
Leave a comment