CHAMA cha Wananchi (CUF), kimemuomba Rais Samia Suluhu Hassan, atembee katika maneno yake kuhusu upatikanaji wa maridhiano ya kitaifa Kwa kuhakikisha Tume Huru ya Uchaguzi, inapatikana kabla ya chaguzi zijazo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari, leo Jumanne, tarehe 1 Novemba 2022, jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa CUF Taifa, Profesa Ibrahim Lipumba, amesema suala la upatikanaji tume hiyo na katiba mpya, linapaswa kupewa uzito.
“Kutengeneza tume huru ya uchaguzi inahitaji miaka miwili mitatu kabla ya uchaguzi wenyewe, ndiyo maana nililalamika kuchelewa kwa Kikosi Kazi cha Rais kufikisha mapendekezo yetu kwa Rais Samia.
Tunamuomba Rais atembee kwenye maneno yake aliyozungumza asisubiri mpaka watu wakate tamaa,” amesema Prof. Lipumba.
Prof. Lipumba amesema, chama chake kinapendekeza Uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa 2024 na Uchaguzi Mkuu wa 2025, zifanyike chini ya usimamizi wa Tume Huru ya Uchaguzi, inayotokana na maoni ya wananchi yaliyoratibiwa na Tume ya Waziri Mkuu Mstaafu, Jaji Joseph Warioba.
“Tunaishauri Serikali kwa mambo nyeti hasa suala la kupata tume huru ya uchaguzi yaweze kushughulikiwa haraka kusudi tuweze kirekebisha taratibu za chaguzi,” amesema Prof. Lipumba.
Aidha, Prof. Lipumba amemuomba Rais Samia akamilishe mchakato wa marekebisho ya katiba, Ili ipatikane mpya.
Leave a comment