WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewataka watumishi wa umma kufanya kazi kwa weledi, uaminifu na uadilifu ili waweze kuleta matokeo chanya katika sekta mbalimbali za kimaendeleo na hawapaswi kuwa wala rushwa. Anaripoti Victoria Mwakisimba,TUDARCo … (endelea).
Pia, amewataka watumishi hao wahakikishe wanafanyakazi ya kutoa huduma kwa wananchi kwa kufuata taratibu zilizowekwa pamoja na kusimamia vizuri fedha za miradi ya maendeleo zinazopelekwa katika maeneo yao.
Ameyasema hayo leo Jumamosi, tarehe 18 Septemba 2021, wakati akizungumza na watumishi wa umma wilayani Kibondo wakati akiwa katika ziara ya kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo na shughuli za kijamii mkoani Kigoma.
Amesema Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan anatarajia kuona mipango yote ya Serikali inatekelezwa katika jamii kwani kufanya kazi kwa bidii kutasaidia wananchi kujishughulisha na mambo mengine ya maendeleo.
“Wito wa Rais Mheshimiwa Samia ni kuona uchumi unaenda kwa kasi kuanzia mtu mmoja mmoja, jamii na taifa kwa ujumla, tulianza na ujenzi wa miundombinu mbalimbali ili kuwawezesha watanzania kufanya shughuli zao za kiuchumi,” amesema Majaliwa.
Amewataka watumishi hao kuwahamasisha na kuwawezesha Watanzania kujishughulisha shughuli za kiuchumi.
“Kama ni mkulima alime sana, kwenye migodi wafanye kazi sana, wanafanyabiashara wafanye sana biashara hata wanaosoma wasome sana”
Amesema watumishi washiriki kikamilfu katika kusimamia makusanyo ili kuwawezesha kutekeleza miradi wanayoiona italeta tija kwa wananchi. “Kigezo cha ukusanyaji wa mapato kipimwe kutokana na ujenzi wa miradi ambayo inawahudumia wananchi.”
Waziri Mkuu pia amewaagiza Wakuu wa Wilaya wahakikishe kuwa miradi yote inayotekelezwa inakuwa na thamani ya fedha iliyotolewa “Wakurugenzi simamieni utekelezaji wa miradi katika maeneo yenu ili Wakuu wa Wilaya wakija kuizindua ionekane thamani ya mradi huo.”
Leave a comment