Watu takribani 93 wamefariki dunia na wengine zaidi ya 140 wamejeruhiwa baada ya watu wenye silaha za moto kufyatua risasi katika tamasha la muziki wa rock kwenye ukumbi wa Crocus nje kidogo ya jiji la Moscow jana Ijumaa. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa… (endelea).
Taasisi ya kijasusi ya Urusi (FSB) ilitangaza kuwa moto mkubwa ulilipuka katika jengo hilo na kusababisha sehemu ya paa jirani na eneo la kuchezea kuporomoka.
FSB amemwambia Rais Vladimir Putin kuwa watu wanne kati ya 11 waliohusika katika shambulio katika ukumbi huo, tayari wamekamatwa.
Hata hivyo, Kundi la Islamic State limedai kufanya shambulio hilo, na kwamba waliofanya shambulio walikimbia.
Marekani imesema hakuna sababu ya kutilia shaka madai hayo ya Islamic State, Ikulu ya White House ikisema mapema mwezi huu iliionya Urusi kuhusu uwezekano wa kutokea shambulio kwenye “mikusanyiko mikubwa” jijini Moscow.
Licha ya kwamba Urusi bado haijatoa tamko lolote, Ukraine, ambayo kwa sasa ipo vitani na Urusi, imekana kuhusika kwa namna yoyote.
Picha ya video ambayo BBC imeipata inaonesha washambuliaji wakifyatua risasi ovyo dhidi ya raia waliokuwa wakipiga kelele huku wakijaribu kukimbia na milipuko mingi ikisikika.
Ulinzi umeimarishwa huku matukio ya mikusanyiko yakifutwa kote nchini Urusi wakati maafisa wa ulinzi na usalama wa nchi hiyo wakiwasaka washambuliaji.
Rais Putin bado hajahutubia taifa moja kwa moja, lakini kwa mujibu wa naibu wake amewatakia majeruhi uponaji wa haraka.
Leave a comment