Maelfu ya wanawake nchini Marekani wameandamana katika zaidi ya miji 600 nchi hiyo kupinga kampeni ya kuzuia uavyaji (utoaji) mimba. Anaripoti Mwandishi wetu. (endelea…)
Katika jiji la Washington takriban waandamanaji 10,000 walijitokeza karibu na ikulu ya rais, ‘White House’ kabla ya kuelekea katika mahakama ya juu ambayo itatoa uamuzi wa mwisho kuhusu suala hilo tete nchini humo.
Waandamanaji walibeba mabango yenye ujumbe kama ”Ruhusu uavyaji mimba uwe halali kisheria, uavyaji mimba ni suala la afya na afya ni haki ya binadamu.”
Mvutano kuhusu suala hilo nchini Marekani uliibuka Agosti mwaka huu katika jimbo la Texas baada ya kupitisha sheria iliyopiga marufuku uavyaji mimba. Sheria hiyo ilianza kutekelezwa tarehe 1 Septemba 2021.
Tangu wakati huo mashauri mengi yamewasilishwa mahakamani na bungeni, lakini sasa maandamano ndio ymaeanza kushamiri zaidi.
Siku mbili kabla ya mahakama ya juu kuanza vikao, waandaaji wa maandamano hayo wamesema watu waliandamana katika zaidi ya miji 600 na kuongeza kuwa maelfu ya watu walishiriki maandamano hayo katika majimbo 50.
”Wanawake ni wanadamu, sote ni wanadamu na tunahitaji haki kama wanadamu wote,” amesema Laura Bushwitz, mwanamke mwenye umri wa miaka 66 ambaye ni mwalimu mstaafu wa jimbo la Florida aliyeshiriki maandamano hayo.
”Tunapaswa kuwa huru kujifanyia maamuzi yetu wenyewe kuhusu kile tunachotaka kufanya katika miili yetu,” amesema Michaellyn Martinez ambaye anakadiriwa kuwa na umri wa miaka 70.
Katika maeneo ya mahakama ya juu, waandamanaji hao walikabiliwa na waandamanaji wapinzani yaani wanaounga mkono sheria ya iliyopiga marufuku uavyaji mimba.
Hadi sasa ndani ya mwaka huu, majimbo 19 Marekani yameridhia sheria 63 zinazodhibiti huduma za utoaji mimba.
Leave a comment