MAALIM Seif Sharif Hamadi, Mwenyekiti wa Chama cha siasa cha upinzani nchini Tanzania cha ACT-Wazalendo amesema, Hayati Benjamin Willium Mkapa alikuwa jasiri ingawa mengine hakuyapenda. Anaripoti Yusuph Katimba, Dar es Salaam … (endelea).
Rais mstaafu Mkapa amefariki dunia usiku wa kuamkia jana Ijumaa tarehe 24 Julia 2020, katika hospitali moja jijini Dar es Salaam na anatarajiwa kuagwa kuanzia kesho Jumapili katika Uwanja wa Uhuru jijini humo kwa siku tatu hadi Jumanne tarehe 28 Julai 2020.
Soma zaidi:-
Mwili wa Mkapa, aliyehudumu kwa miaka kumi kati ya mwaka 1995 hadi 2005 utazikwa kijijini kwake Lupaso, Masasi Mkoa wa Mtwara Jumatano tarehe 29 Julai 2020.
Maalim Seif amesema, miongoni mwa mambo yaliyomfanya Mkapa kuwa wa kipekee ni kuwa na msimamo na lile analoliamini lakini pia kulisema waziwazi.
Akizungumza akiwa nyumbani kwa Mkapa, Masaki jijini Dar es Salaam leo Jumamosi tarehe 25 Julai 2020, amesema wakati anatia saini maridhiano ya Zanzibar mwaka 2001 alisema Tanzania si mali ya mtu.
“Kwa hiyo, ni mtu alikuwa stable (imara), anajiamini. Pamoja na mengine ambayo sisi wengine tulikuwa hatuyapendi lakini mimi namuheshimu kwa msimamo wake,” amesema Maalim Seif, Makamu wa Kwanza wa Rais mstaafu wa Zanzibar
“Alikuwa stable (imara) na hayumbi. Wakati wa kutia saini mwaka 2001 alisema waziwazi kwamba, Tanzania si mali ya mtu ama kikundi cha watu na hakuna chama chenye hati miliki, Tanzania ni ya Watanzania,” amesema Maalim Seif.
Amemtaja Mkapa kuwa ni miongoni mwa watu walioshiriki na kusukuma kufanikiwa kwa maridhiano mwaka huo baada ya mauaji yaliyotokea Pemba tarehe 26 na 27 Janauari 2001.
“Alifayanya kazi kweli kuhakikisha ule mwafaka unafikiwa, alikuwa akinialika nyumbani kwake kaika hatua za kuleta muafaka Zanzibar.
“Kwenye kamati zilizokuwa zikishughulikia mwafaka, tulikuwa tunaona mambo mazuri, alikuwa akizungumza kwa dhati na anaonesha usoni kwamba anamaanisha kile anachozungumza,” amesema Maalim Seif.
Kiongozi huyo nguli visiwani Zanzibar amesema, Mkapa aliingia madarakani akiwa amejitayarisha kuongoza na kwamba, ndio maana alikuwa mtu anayejiamini, haogopi kusema hata kama anajua watu wengi hawatakipenda.
“Maoni yake anayatoa bila woga, kwa hivyo hizo ndio quality (sifa) za kiongozi wa taifa, maana yeye ndio anaongoza. Haongozi na watu wanataka nini, anaongoza kwa ule muono wake. Yeye alikuwa akiongozwa na muono wake,” amesema.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online na MwanaHALISI TV kwa habari mbalimbali
Leave a comment