MWENYEKITI wa Chama Cha CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amemteua Rashid Sudi Khamis, kuwa Naibu Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma wa chama hicho huku Nawiya Abdallah Mussa, akiteuliwa kuwa Naibu Mkurugenzi wa Fedha na Uchumi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea)
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Jumatatu, tarehe 12 Septemba 2022 na Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma wa CUF, Mhandisi Mohamed Ngulangwa, uteuzi wa wakurugenzi hao utakamilika baada ya wahusika kuthibitishwa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la chama hicho.
“Mwenyekiti wa CUF, Prof. Lipumba baada ya kushauriana na makamu wake na kwa kuzingatia masharti ya Ibara ya 94 ya Katiba ya CUF, toleo la 2019, amefanya uteuzi wa wakurugenzi wawili,” imesema taarifa ya Mhandisi Ngulangwa.
Taarifa ya Mhandisi Ngulangwa imesema, Khamis ameteuliwa kushika nafasi hiyo baada ya aliyekuwa anaishika, Mbarouk Seif Salum, kuteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar.
Naye Nawiya amteuliwa kuwa Naibu Mkurugenzi wa Fedha na Uchumi, kushika nafasi ya Khadija Makontena aliyefarikia dunia.
Leave a comment