RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amesema kuna haja ya vijana wa Afrika kuweka msukumo zaidi katika matumizi ya sayansi na teknolojia katika kutatua changamoto na kukuza uchumi wa bara hilo.Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Ametolea mfano nchi ya China ambapo amesema vijana wenye umri wa kuanzia miaka 18-35 ndiyo wamekuwa chachu katika mapinduzi ya viwanda nchini humo kwa kutumia sayansi na teknolojia.
Mkuu huyo wa nchi ameyasema hayo leo Jumatatu tarehe 12 Septemba, 2022, wakati akifungua Kongamano la Wanawake na Vijana katika eneo Huru la Biashara Afrika litakalofanyika kwa siku tatu jijini Dar es Salaam.
Rais Samia ambaye aliteuliwa na Umoja wa Afrika kuwa kinara wa kuhamasisha wanawake na vijana wa Afrika kushiriki biashara, amesema ni muhimu vijana wa Afrika kujengewa uwezo wa matumizi ya sayansi na teknolojia ili kukoa kiasi kikubwa cha fedha ambacho kinatumika kuajiri vijana wa nje ya Afrika.
“Ni muhimu wakajengewa vijana wa Afrika uwezo ikiwemo kutumia sayansi na teknolojia itakayowawezesha kuleta maendeleo kwa uimara wa uchumi wa Afrika,” amesema na kuongeza;
“Mfano China uchumi wake unajengwa na vijana wa umri wa miaka 18-35 nasi tukijiendeleza huko Afrika tuna vijana wengi ambao wanaweza kujenga uchumi wetu kwa kutumia sayansi na teknolojia.”
Samia litoa wito kwa Kongamano hilo kuja na mapendekezo na mikakati madhubuti ya kuimarisha uwezo wa vijana na wanawake wa Afrika.
“Tuendelee kuwekeza zaidi katika rasilimali watu hususani wanawake na vijana. Tukiwa na nguvu kazi imara ni rahisi zaidi kutumia rasilimali zilizopo kujiletea maendeleo,” amesema.
Amesema kukosekana kwa ujuzi wa kutosha Afrika inasababisha utegemezi wa mabara mengine kuja kutumia rasilimali za Afrika na hivyo kuwanufaisha wao zaidi.
Leave a comment