JAKAYA Mrisho Kikwete, Rais mstaafu wa Tanzania, amewataka wagombea wa Chama cha Mapinduzi (CCM) katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano wa tarehe 28 Oktoba 2020, kutonyimwa usingizi na maneno ya vyama vya upinzani. Anaripoti Mwandishi Wetu, Chalinze … (endelea).
Kikwete ametoa kauli hiyo leo Alhamis tarehe 3 Septemba 2020 katika uzinduzi wa Kampeni za CCM wilayani Chalinze mkoa wa Pwani, ambao umefanywa na Samia Suluhu Hassan, Mgombea mwenza wa urais wa Tanzania kupitia CCM.
Mwanasiasa huyo amesema, maneno ya kwamba mambo ni magumu ndani ya CCM siyo kweli, hivyo yasiwakatishe tamaa.
“Maneno ya watani zetu yasiwape jakamoyo, yasiwanyime usingizi, yasiwakatishe tamaa mkadhani kwamba mambo ni mabaya siyo kweli na hawatakaa watusifie,” amesema Kikwete.
Kikwete amesema, vyama vya upinzani havitashida uchaguzi huo kwa madai havina nguvu na wanachama wa kutosha hususan katika Jimbo la Chalinze ambalo mgombea ubunge ni mwanae, Ridhiwan.
“Hapana shaka vyama vitakuwepo tu na vimekuwepo muda mrefu, nilipokuwa mbunge (wa Chalinze) tuligombea wengi na wengine unagombea nao wanakwambia mzee mi narudisha fomu, namwambia rudisha anarudia tena, namwambia we si wa chama kingine? Uliza viongozi wa chama chako,” amesema Kikwete.
Kikwete aliyeongoza Tanzania kwa miaka kumi kati ya 2005 hadi 2015, ametumia fursa hiyo kumwombea kura John Magufuli, mgombea Urais wa CCM, akisema Ilani ya uchaguzi ya chama hicho imebeba mikakati ya mafanikio kwa miaka mitano ijayo.
“Ilani yetu ya uchaguzi mi nimeisoma inatupeleka huko, inatutoa hapa tulipo na kutupeleka mahali pazuri zaidi miaka mitano ijayo. Hakuna sababu wananchi wasimchague tena rais wetu,” amesema Kikwete.
“Siku moja nilikuwa nazungumzana rafiki yangu mmoja yuko chama cha upinzani, nikamuuliza ndugu yangu hivi kwa nini siku zote hakuna jema CCM imefanya? Akaniambia sikiliza, kazi yakujisifia yenu nyie sio yetu, sio kwamba hatuoni, ila tukiwasifia watatuuliza kwa nini tuko upande huu,” amesema Kikwete.
Leave a comment