DUNIA imelaani hatua ya mwanajeshi wa Jeshi la Israel, kumkandamiza kwa kifuti cha mguu kwenye shingo ya muandamanaji wa Palestina. Inaripoti Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC).
Picha ya tukio hilo ilisambazwa kwenye mitandao ya kijamii, imesababisha jeshi hilo kutuhumiwa kwa ukiukwaji wa haki za binadamu.
Tukio hilo linafanana nalile lililotokea nchini Marekani, ambapo George Floyd, Mmarekani mweusi aliuawa baada ya kuwekewa kifuti kwenye shingo yake, tukio hilo liliibua vurugu nchini humo na kulaaniwa duniani kote.
Video ya tukio hilo la mwanajeshi wa Israel yenye sekunde 50, inamuonesha Khairi Hanoon, mwanaharakati wa Palestina akiwa amelazwa chini kisha mwanajeshi huyo akimwekea kifuti kwenye shingo yake.
Pia, tukio hilo limelaaniwa na utawala wa Palestina huku, Israel katika maelezo ya awali imeeleza mwanajeshi huyo alifanya tukio hilo kwa tahadhari.
“Futi hilo liliwekwa juu juu na haliwezi kumaanisha ni tukio la uvunjaji wa haki uliofanywa na jeshi,” imeeleza taarifa ya awali.
Video hiyo iliyozidisha hasira za Wapalestina, ilichukuliwa kwenye maandamano eneo la West Bank katika Kijiji cha Shufa, Jumanne wiki hii.
Kwa mujibu wa Sheria za Kimataifa, eneo hilo ni mali ya Palestina lakini limekaliwa kimabavu na Israel.
Leave a comment