WANAVIJIJI kutoka kata nne za Wilaya ya Musoma Vijijini, mkoani Mara, wako mbioni kuondokana na adha ya huduma ya maji safi na salama baada ya miradi yake inayotarajiwa kukamilika hivi karibuni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mara…(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Ofisi ya Mbunge wa Musoma Vijijini, Prof. Sospeter Muhongo, miradi ya ujenzi wa miundombinu ya kusambaza maji kutoka Ziwa Victoria, ipo mbioni kukamilika.
Taarifa hiyo imesema kuwa, mitambo ya kusukuma maji inayotengenezwa katika nchi za China, Hungary na Turkey, inatarajiwa kuwasilisha nchini kupitia mradi wa bomba kuu la maji la Mugango-Kiabakari-Butiama, unaogharimu Sh. 70.5 bilioni.
“Mradi huu uwezo wake wa kuzalisha maji ni Lita 35 milioni kwa siku. Katika Kata za Tegeruka na Mugango, Mbunge alienda kukagua ujenzi huo,” imesema taarifa hiyo.
Mbali na ujenzi wa mabomba ya kusambaza maji, pia ujenzi wa matenki ya maji unaendelea jimboni humo, ikiwemo tenki lenye ujazo wa Lita 135,000 linalojenhwa katika Kijiji Cha Kataryo.
“Wananchi wa Jimbo la Musoma Vijijini wanaishukuru Serikali yetu chini ya uongozi mzuri wa Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maji ya bomba vijijini mwetu,” imesema taarifa hiyo.
Leave a comment