IDDI Azzan, aliyekuwa Mbunge wa Kinondoni (CCM), anajipanga kumvaa Maulid Mtulia anayemaliza muda wake kwenye jimbo hilo, jijini Dar es Salaam. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, Azzan alishindwa na Mtulia, wakati huo akiwa Chama cha Wananchi (CUF). Mtulia alihama CUF na kujiunga na CCM na kisha kugombea tena ubunge jimbo hilo na kushinda.
Azzan ametoa kauli hiyo jana tarehe 5 Julai 2010 katika mahojiano maaulum na MwanaHALISI Online, alipoulizwa kuhusu dhamira yake ya kurejea kwenye ulingo wa siasa. Azzan alihudumu kwenye jimbo hilo kwa vipindi viwili mfululizo – 2005/2010 na 2010/2015.
Azzan amesema, anataka kugombea tena kwenye jimbo hilo ili amalizie miradi aliyoianza wakati akiwa mbunge.
Soma zaidi:-
“Yapo mambo mengi yamenifanya niwe na azma ya kurudi bungeni, kubwa ni kutekeleza yale niliyotamani nitekeleze mikononi mwangu.
“Nataka nipambanie niliyokusudia kipindi hicho, naona kuna haja ya kuwatumikia, sisemi ubunge ni kama kazi, tayari ninashughuli zangu lakini ni wito wa kutumikia wananchi kutoka moyoni,” amesema Azzan.
Amesema, ana imani kwamba wananchi wa Kinondoni bado wanamuhitaji na pia kuhitaji utumishi wake.
“Kwanza niseme, ule uchaguzi wa 2015 kulikuwa na upepo fulani ulipita, lakini naamini wananchi wa Kinondoni bado wanahitaji huduma yangu. Kinondoni nilipokulia, nilishiriki mambo mengi ya kijamii, mimi ni mtoto wa Kinondoni,” amesema Azzan.
Wakati huo huo, Azzan amesema anataka apate fursa ya kunadi mazuri aliyoyafanya Rais John Magufuli, katika uongozi wake kupitia kampeni za uchaguzi.
“Sikufichi, ndio ameanza lakini tunaona mambo makubwa na maendeleo makubwa ameyafanya, suala la kusema unampenda Magufuli halafu unakaa ndani haisaidii, inatakiwa upate jukwaa uelezee mazuri ya yake kwa wananchi,” amesema Azzan.
Leave a comment