UMOJA wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umesema, katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020, jimbo la Iringa Mjini watashinda asubuhi na mapema. Anaripoti Mwandishi Wetu, Iringa … (endelea).
Pia, UVCCM imewaonya wanachama wa chama hicho hususan waliotia nia kuwania ubunge wa jimbo hilo kuwa kitu kimoja na atakayepitishwa na chama aungwe mkono na wote ili kuepusha mpasuko.
Hayo yalisemwa jana Jumapili tarehe 5 Julai 2020 na Katibu Mkuu wa UVCCM, Raymond Mwangwala wakati akikabidhi vyeti kwa wanachuo wa vyuo vikuu na seneti ya vyuo vikuu Mkoa wa Iringa.
Alisema kile kilichofanywa na Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli ndiyo turufu ambayo wananchi wapo tayari kuichagua CCM.
Mwangwala alisema, utafiti ambao waliufanya ulionyesha miongoni mwa majimbo ambayo watashinda mapema ni hilo la Iringa Mjini ambalo linaongozwa kwa miaka kumi mfululizo na Mchungaji Peter Msigwa wa Chadema.
“Ninachoweza kusema, ninyi wanaCCM, msivuruge huo utaratibu wa chama, acheni kufitiniana ninyi kwa nyingi hususani wagombea mnaotaka kugombea,” alisema.
“Atakayeshinda mmuunge mkono, hili jimbo CCM tumeshalichukua na hii ni habari ya majimbo yote ya upimbani, tunakwenda kuyachukua,” alisema Mwangwala.
Katibu huyo alisema, ni heri tupigane kwa hoja ndani ya chama kuliko kuwa na upinzani unaobebwa na mabeberu.
“Tutabakia sisi wenyewe kujenga hoja ndani kwa sababu hata katika vikao vyetu, tunanafasi ya kusema hiki kiende hiki kisiende kwa sababu kinamanufaa ya wananchi na taifa kwa ujumla,” alisema Mwangwala.
Katibu mkuu huyo alitumia fursa hiyo, kuwataka wanachuo hao kuwa watulivu wanapoelekea kwenye kura za maoni ili wakatumie demokrasia yao kwa utulivu.
“Atakayeshinda yeyote katika kura za maoni ni kazi yetu wanachama kuhakikisha tunamuunga mkono na kuhakikisha anapeperusha bendera ya Chama cha Mapinduzi.”
“Msije mkatumia fedha mkidhani mtapita, hata atakayeshinda namba moja, tutaingia kwenye mjadala tujue ameshindashindaje,” alisema.
Awali, Katibu wa CCM Mkoa wa Iringa, Brown Mwangomale alisema, alitoa ushauri kwa wanaotaka kugombea kujipima kwanza kuliko kusikiliza kile wanachoelezwa na watu kwamba wakagombee.
Mwangomale alisema,“Julai 20 nimeagiza gari za wagonjwa za halmashauri zote zije katika ukumbi wa CCM ili mtia nia akidondoka jukwaani baada ya kupata matokea wanambeba wanapeleka hospitali.”
Mwangomale alisema katika jimbo la Iringa anatafutwa mgombea mmoja lakini watia nia wapo 30 hivyo yeyote atakayeona amepata kura 0 aweke mikono mfukoni atoke akiwa salama.
“Ukipata kura tano tano ukaona kwa mwenzio zinajaa usipaniki mwaka huu tunataka uwazi, ili ukianguka wale waliokuwa wasema ni wewe tu ukawaulize mbona mlisema ni mimi tu alafu nimetoka na 0?”
“Bahati nzuri wapiga kura wanakupa matumaini mazito sana, kabla hujatiania jipime mwenyewe je unaweza,” alisema.
Katibu huyo aliwataka wagombea kuacha kuchukulia kirahisi suala la kugombea lakini wakiamua kugombea waende wakagombee kwa moyo mweupe wafikirie kuna kushinda na kushindwa.
Naye, Mwenyekiti wa seneti ya vyuo vikuu Iringa, Emmanuel Mlelwa walimpongeza Rais John Magufuli kwa kuwasaidia vijana kupata ajira rasimi na zisizo rasimi ili kuondokana na tatizo la ajira nchini.
Mlelwa alisema, wao kama wanachuo walifanya utafiti na kuwaunganisha wanachuo pamoja na jamii lengo kubwa likiwa ni kuwaweka wananchi pamoja.
Leave a comment