RAIS wa Zanzibar, Dk. Hussein Mwinyi, amewataka waandishi wa habari visiwani humo, kuandaa namna bora ya kuunda sheria mpya ili kuimarisha sekta hivyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Dk. Mwinyi ametoa kauli hiyo leo Jumatatu tarehe 1 Machi 2021, wakati akizungumza kwenye Kongamano la wanahabari visiwani humo.
“Kadhalika katika kongamano hili mtaweza kutoa maoni yenu ya kina na mapendekezo kuhusiana na sheria ya habari kwa serikali, kwa lengo la kupata sheria ambayo itaweza kutumika kuimarisha zaidi sekta ya habari nchini na kuongeza mchango wake katika maendeleo ya nchi yetu,” amesema Dk. Mwinyi.
Dk. Mwinyi amesema, matarajio yake ni kuwa kongamano hilo, litaibuka na mbinu bora zitazoweza kutumika katika kuandaa utoaji bora wa taarifa.
“Ni matumaini yangu, katika majadiliano yenu mtaweza kutoka na mikakati ya pamoja na mbinu zitakazoweza kutumika katika kuandaa namna bora ya utoaji wa taarifa kwa wananchi.

“Taarifa zitakazohusu utendaji katika ofisi za serikali, kuhusiana na utekelezaji wa miradi mbalimbali kwa mujibu wa mipango mikuu ya serikali, ikiwemo dira ya maendeleo ya 2020 hadi 2050,” amesema.
Rais huyo ameeleza, miongoni mwa changamoto alizokutananazo katika siku chache baada ya kuwa rais, ni pamoja na serikali kutokuwa na mfumo wa kupokea changamoto za wananchi na kuzifanyia kazi.
Amesema, wananchi wamekuwa na changamoto nyingi katika maisha yao, lakini mfumo wa serikali ulioimarishwa na wa kupeleka taarifa kwa wananchi na si kupokea.
“Miongoni mwa mambo niliyobaini katika kipindi hiki kifupi baada ya kuchaguliwa kuwa Rais wa Zanzibar, ni changamoto nyingi zinazowakabili wananchi na kwa bahati mbaya, wanakosa sehemu ya kuziwasilisha changamoto hizo na kupata ufumbuzi wa haraka.
“Kwa muda mrefu tumeimarisha mifumo yetu kupeleka taarifa kwa wananchi, lakini ka bahati mbaya hatukuimarisha mifumo ya kupata taarifa kutoka kwa wananchi,” amesema.
Na kwamba, serikali yake imeamua kuanzisha mfumo mpya wa kupokea taarifa moja kwa moja kutoka kwa wananchi, mfumo huo – Sema Na Rais (SNR Mwinyi), mfumo huo ulizinduliwa Jumamosi wiki iliyopita.
SNR Mwinyi
Hongera sana Rais Mwinyi kwa kuanzisha mfumo huu maridhawa. Ningeshauri na Rais Magufuli naye awe anaonana na waandishi angalao kila mwezi