MKUU wa Wilaya ya Nzega, ACP Advera Bulimba amesema kiasi cha Sh bilioni 24.4 ambacho fedha za mapambano ya Uviko-19 zilizopelekwa kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika wilaya hiyo, zimewawezesha wazawa kupiga hatua kiuchumi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumzia miradi inayotekelezwa katika wilaya hiyo, Bulimba amesema tangu Rais Samia Suluhu Hassan aingie madarakani wilaya hiyo imepokea fedha nyingi kutekeleza miradi ya maendeleo.
“Hizi Sh bilioni 24.4 ziko kwenye mzunguko wa wananchi wa kawaida kabisa kwa sababu tulitumia mafundi wazawa katika utekelezaji wa miradi yote.
“Hali ya maisha ya wananchi wetu wa Nzega imeboreshwa kwani kila mwananchi alikuwa na uwezo wa kupata hiyo pesa, kama hukushiriki kwenye miradi ya barabara, basi alishiriki kuwa kibarua kwenye mradi wa maji, vituo vya afya, ujenzi wa madarasa na miradi mingine bado inaendelea na wananchi wanaendelea kunufaika na hizi pesa,” amesema.
Kauli hiyo imeungwa mkono na Mkurugenzi Halmshauri Nzega, Shomary Mndolwa ambapo amesema fedha zikishapokelewa zinaundiwa kamati ambazo zinahusisha wananchi.
“Kuna kamati za ujenzi, manunuzi ambazo zote zinakuwa na kitu kimoja cha kumiliki mradi na kuusimamia.
“Pia pesa hizi zinatumika kwa sehemu husika hivyo mafundi wazawa wanafaidika na hizo pesa, tunatumia wazabuni wa ndani ya halmashauri ambao pia wamefaidika na mradi huo,” amesema.
Pia amemshukuru Rais Samia kwa kuongeza mzunguko wilayani hapo hasa katika kipindi hiki cha ujenzi wa vituo vya afya.
Aidha, mmoja wa mafundi ujenzi waliofaidika na miradi hiyo Mabula Busongo amesema mpango madhubuti wa kutumia mafundi, vibarua wazawa umekuwa chache kwa maendeleo ya wananchi wilayani hapo kwani fedha hazijaondoka.
Amesema hadi sasa fedha aliyoipata imemuwezesha kununua ng’ombe watatu.
Leave a comment