WIZARA ya ulinzi nchini Tanzania imekusanya maduhuli yake kwa asilimia 1,288.95 baada ya kukusanya kiasi cha Sh 15.4 milioni kati ya Sh 1,200,000 zilizopangwa kukusanywa katika mwaka wa fedha 2021/22. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Makusanyo hayo ni ya fungu 57 linalohusu Wizara ikiwa ni moja ya mafungu matatu ya Wizara hiyo.
Takwimu hizo zimebainishwa leo Alhamisi tarehe 19 Mei 2022 na Waziri wa Ulinzi, Dk. Stergomena Tax, wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2022/23.
“Wizara, imekusanya Shilingi 15,467,440.50 sawa na asilimia 1,288.95 ya makadirio, zilizotokana na huduma ya Mtandao wa Mawasiliano Salama na mapato ya Ulinzi Channel iliyopo kwenye mtandao wa YouTube,” amesema Dk. Tax.
Hata hivyo kwa ujumla ya mafungu yote Wizara imefanikiwa kukusanya maduhuli ya Sh. 120.5 milioni sawa na asilimia 141.66 ya makadirio ya Sh. 85.1 milioni.
Amesema kwa upande wa Fungu 38 : Ngome, yamekusanywa maduhuli yenye jumla ya Sh. 43.1 milioni sawa na asilimia 196.32 ya makadirio, yanayotokana na mauzo ya nyaraka za zabuni, na malipo ya kamisheni zinazotokana na makato ya bima kwa wanajeshi kutoka makampuni mbalimbali ya bima.
Ameongeza Fungu 39 : JKT limekusanya Sh. 61.9 milioni sawa na asilimia 99.99 ya makadirio, zilizotokana na mauzo ya nyaraka za zabuni, mauzo ya mazao ya bustani (mboga mboga na matunda), bidhaa za mifugo, nafaka na bidhaa zitokanazo na ufugaji wa nyuki.
Leave a comment