JOEL Mwinza (44), Daktari Bingwa wa Mifupa kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili kitengo cha Mifupa (MOI), Joel Mwinza ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni, Dar es Salaam jinsi alivyomtibu Deogratus Minja aliyedaiwa kushambuliwa kwa nyundo na mfanyakazi wa Benki ya CRDB, Ibrahim Masahi. Anaripoti Faki Sosi…(endelea).
Dk. Mwinza amedai kuwa alipompokea Minja alikuwa na majeraha kichwani, mgongoni, mkononi na pia kuna sehemu alikuwa amechanika kisogoni, kwa hiyo alitumia mashine ya X-ray na CT Scan kumchunguza mwili wake.
Mtaalam huyo alidai hayo jana Jumanne mbele ya Hakimu Mkazi, Amos Rweikiza wakati akitoa ushahidi wake dhidi ya Masahi anayetuhumiwa kumshambulia kwa nyundo Minja tarehe 11 Januari 2023 eneo la Mbezi Msakuzi, Dar es Salaam.
Alidai kuwa tarehe 24 Januari 2023 alimpokea mgonjwa Deogratus ambaye alipelekwa kwake na daktari kutoka Kitengo cha dharura cha wagonjwa MOI akiwa na historia ya kujeruhiwa na jirani yake. Mgonjwa huyo alipelekwa kwa daktari huyo ili amtibu shida ya mifupa.
“Alikuwa ana majeraha kichwani, mgongoni, mkononi, alikuwa amechanika kichwani ameshonwa nyuzi na pia bega la kulia lilikuwa na maumivu, nilimfanyia vipimo, X-ray ilionesha amevunjika bega na CT Scan ilionesha ameumia kwenye ubongo,” alidai Dk. Mwinza
Alidai kuwa baada ya vipimo, akaanza kumpatia matibabu, kwa kumuandikia dawa na katika tatizo la bega alimpa kifaa tiba ambacho alikitumia kwa muda wa wiki sita na kwa upande wa majeraha yaliyoshonwa yalisafishwa na kutolewa nyuzi.
“Mgonjwa alinipa fomu ya polisi Pf3 nikaijaza, nikampangia siku kwamba baada ya wiki mbili arudi tena MOI kwa ajili ya uchunguzi. Sikumbuki tarehe, lakini nakumbuka niliitwa na uongozi ili nitoe ushirikiano kwa polisi kuhusiana na mlolongo wa matibabu niliyompa Deogratus,” alidai.
Dk. Mwinza aliendelea kudai kuwa daktari mwenzake alimpokea Minja tarehe 12 Januari 2023, akiwa amepewa rufaa kutoka Hospitali ya Bochi, baada ya kudai hayo aliiomba mahakama ipokee fomu hiyo kama kielelezo katika kesi hiyo, ambapo mahakama ilikipokea kwa sababu Wakili wa utetezi, Nestory Wandiba hakuwa na pingamizi.
Katika ushahidi wake, Minja alidai kuwa tarehe hiyo saa 2:30 usiku alikuwa akipita nje ya geti la jirani yake Masahi ambapo alimkuta kijana wa jirani huyo, baada ya kumuona kijana huyo alizungumza kwa ki-lugha kwa sauti kubwa ambayo yeye hakuielewa.
“Ghafla kijana alikuja mbele yangu akanizuia nisipite, mara geti likafunguliwa akatoka Masahi akanihoji kwamba mimi ni kama nani na kwenda kumshtaki Serikali za mitaa, sikumjibu chochote kijana wake akanipiga ngumi.
“Nilimgeukia jirani yangu ili amuonye kijana wake, lakini na yeye aliinua shati lake akatoa nyundo akanipiga nayo kichwani baada ya kupata maumivu makali nilianza kukimbia huku nikipiga kelele za kuomba msaada,” alidai Minja.
Alidai kuwa, alianguka chini ndipo Masahi akaanza tena kumshambulia na nyundo mgongoni, maumivu yalipomzidi aligeuka, akampiga na nyundo kwenye mkono wa kulia na kwenye bega.
Jirani mmoja alifungua geti na kumsaidia kwa sababu alikuwa anavuja damu nyingi walimpeleka Hospitali ya Bochi kwa matibabu.
Hakimu Mkazi, Amos Rweikiza aliahirisha kesi hiyo hadi tarehe 16 Januari 2024.
Leave a comment