VYAMA vya siasa vinavyoshiriki uchaguzi mdogo wa udiwani katika Kata ya Kiwanja cha Ndege, Manispaa ya Morogoro vimeonywa, anaandika Christina Haule.
Vyama hivyo vimetakiwa kujiepusha na vitendo vya vurugu wakati huu wa kampeni za udiwani zinazotarajiwa kukoma tarehe 21 Januari mwaka huu ambapo tarehe 22 Januari uchaguzi utafanyika.
Wito huo umetolewa na Dk. Steven Kebwe, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro alipozungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana.
Amesema kuwa, mkoa huo hautavumilia kuona chama chochote kinakiuka masharti ya uchaguzi huo kwa namna yoyote ile.
Dk. Kebwe amewashauri wananchi kuwa watulivu katika kipindi cha kampeni na kuwataka kusikiliza maelezo yanayotolewa na vyama vyote ili waweze kuchagua kiongozi watakayemuona anafaa kuwaletea maendeleo ya kweli.
Wakati huohuo Dk. Kebwe amesema kuwa, zoezi la upigaji chapa mifugo linatarajiwa kuanza kufanyika tarehe 1 Februari mwaka huu baada ya mwanzo kusitishwa kutokana na jamii ya wafugaji kutoa ushirikiano wa kutosha na baadhi ya mifugo kudaiwa kuumia kutokana na chapa hizo.
“Zoezi hili ni utekelezaji wa agizo la waziri mkuu kwa barua kumbukumbu namba PM/P/2/569/42, hivyo tunaomba ushirikiano toka kwa makundi yote, ndugu zetu wafugaji na wananchi wote wa mkoa wa Morogoro,” amesema.
Leave a comment