RIPOTI ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere, kwa mwaka wa fedha wa 2022/23, imeibua madudu katika halmashauri 10 na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Bohari Kuu ya Dawa (MSD). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Madudu hayo yamebainishwa na CAG Kichere, wakati akikabidhi ripoti ya ukaguzi wake kwa mwaka wa fedha wa 2022/23 kwa Rais Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 28 Machi 2024, jijini Dodoma.
Kwa upande wa halmashauri, CAG Kichere amesema ukaguzi wake umebaini mamlaka za serikali za mitaa 10 zililipa kiasi cha Sh. 2.9 bilioni kwa kazi zilizotekelezwa bila kuwepo nyaraka zinazoonesha ukubwa wa kazi, wakati mamlaka nne zikilipa Sh. 346.6 milioni kwa kazi ambazo hazikutekelezwa kutokana na kukosekana usimamizi wa miradi.
Pia, CAG Kichere amesema ukaguzi wake umebaini Serikali imeingia hasara ya Sh. 222.3 bilioni kwa kufanya matumizi yasiyokuwa na tija kwa kulipa faini kwa kuchelewesha malipo ya wakandarasi wanaojenga barabara.
Kwa upande wa MSD, CAG kichere amesema “ukaguzi umebaini MSD ilitoa zabuni ya vifaa vya maabara vya UVIKO-19 kwa kampuni ambayo haikuwa na uwezo wa kuvitengeneza hivyo vifaa vilivyofika wataalamu waligundua havifai kwa mashine zetu, hata hivyo MSD ililipa fedha zetu.”
Kuhusu TANESCO, CAG amesema ukaguzi wake umebaini dosari katika zoezi la ubadilishaji wa mita ambapo mita zaidi ya 100,000 kati ya mita 602,266 zilibadilishwa kabla ya kipindi cha uhai wa matumizi yake kuisha, wakati 13,493 zilibadilishwa ndani ya mwaka mmoja baada ya kufungwa, huku zaidi ya 90,000 zikiwa na muda mfupi wa matumizi kinyume na muda unaokubalika wa miaka 20.
“Kubadilisha mita mapema kunasababisha gharama kubwa kwa shirika letu, napendekeza wizara ichunguze sababu za TANESCO kubadilisha mita mapema na kuchukua hatua ili kupunguza gharama za uzalishaji,” amesema CAG Kichere.
Leave a comment