MTANDAO wa watetezi wa haki za mazingira nchini Tanzania, umeundwa kwa ajili ya kuweka mikakati ya kuimarisha shughuli zao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Mtandao huo umeundwa katika warsha ya siku mbili iliyofanyika wiki hii jijini Dar es Salaam kwa wawakilishi wa asasi za kiraia 30 zinazojishuhulisha na masuala ya utetezi wa haki za mazingira. Warsha hiyo iliandaliwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC) na Shirika la Defend Defenders kutoka nchini Uganda.
Afisa Uchechemuzi wa THRDC, Nuru Maro, alisema mtandao huo umeundwa kwa ajili ya kuweka mazingira wezeshi dhidi ya watetezi hao, ili waweze kusaidia katika mapambano ya kukabiliana na athari zinazosababishwa na uharibifu wa mazingira.
“Bila kutambua kazi wanazofanya watetezi wa haki za mazingira, haki zinaweza kupotea hivyo ni lazima kuwajengea uwezo na kuhakikisha mtandao wao unakuwa imara. Kumekuwa na uharibifu mkubwa wa mazingira na kuathiri jamii, tumeamua kutengeneza mtandao huu ambao utasukuma zile ajenda na kuhakikisha mazingira yanalindwa kwa ajili ya maendeleo endelevu,” alisema Maro.
Naye Erick Luwongo kutoka SAhirika la Haki Madini, alisema kwa sasa watetezi wa haki za mazingira wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo hatari ya kufanyiwa mashambulizi na unyanyasaji kutoka kwa wale wanaoshukiwa kuwa waharibifu wa mazingira.
Luwongo alisema mtandao huo utasaidia kulinda haki zao pamoja na kuwatetea wanapokuwa katika matatizo.
Leave a comment