KATIKA kuongeza wigo kwa wawekezaji na wafanyabiashara kurasimisha biashara zao, Wakala ya Usajili wa Biashara na Leseni nchini (BRELA) umetoa wito kwa wafanyabiashara hao kuchangamkia huduma mbalimbali zinazotolewa na Brela katika maonesho ya sita ya teknolojia ya madini mkoani Geita. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hayo yamebainishwa jana Mjini Geita na Kaimu Mkurugenzi Miliki Ubunifu kutoka Brela, Loy Mhando wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu malengo ya wakala huo katika maonesho hayo yaliyoanza tarehe 20 Septemba mwaka huu.
Amesema katika maonesho hayo wamelenga kutoa elimu kwa wadau wote hasa ikizingatiwa Brela ndio mlango wa kurasimisha biashara nchini.
Amesema iwapo mdau, mwekezaji au mfanyabiashara anaweza kupata huduma za kurasimisha biashara papo hapo katika banda la Brela kisha akaendelea na hatua nyingine.
“Pia tunatoa huduma saidizi pamoja na huduma za kuhuisha usajili wa makampuni ambayo yalisajiliwa kabla ya mfumo kwa sababu huduma zote zinatolewa na Brela, zinatolewa kwa njia ya mtandao,” amesema na kuongeza;
“Mfumo huo wa kutoa huduma kwa njia ya mtandao ulianza kutolewa mwaka 2018. Kwa hiyo zipo kampuni au biashara zilizosajiliwa kabla ya kuanzishwa kwa mfumo wa mtandao hivyo wamiliki wake wanatakiwa kuhuisha,” amesema.
Aidha, Mhando amesema hatua hiyo ni katika kutekeleza agizo la Naibu Waziri wa Viwanda, na Biashara, Exaud Kigahe kwamba taasisi zinazohudumia wafanyabiashara na wawekezaji kuhakikisha zinawawezesha badala ya kuwa kikwazo kwao katika utoaji wa huduma zinazotolewa na Brela.
Amesema wamejipanga kuwawezsha wadau wote wa biashara nchini, kwa kutoa huduma kwa njia ya mtandao hasa ikizingatiwa mfumo huo unapatikana kila mahali nchini.
Aidha, kwa wale wafanyabiashara hawajafikiwa na mfumo huo, Brela imejipanha pia kuwafuata wadau hao huko walipo mikoani au wilayani kuwaelimisha kwani sio wote wanaweza kwenda katika ofisi za Brela.
“Kwa hiyo tunawafuata na kuwaelimisha na kuwaelezea faida ambazo zinatokana na kurasimisha biashara ambazo wanazifanya au wanategemea kuzifanya” amesema.
Akizungumzia wafanyabiashara ambao hawajarasimisha biashara zao, Mhando amesema sio kwamba wanafanya makusudi ila inaonekana wafanyabiashara hao hawana elimu ya kutosha kuhusu urasimishaji huo hivyo Brela imejipanga kuwafuata katika wilaya zote nchini.
Leave a comment