WAKANDARASI wazawa nchini wametakiwa kuacha kufanya kazi kwa mazoea badala yake wafanya kazi zenye viwango bora na tija katika miradi wanayoipata ili waendelee kuaminiwa na serikali.
Pia wameshauriwa kutambua kuwa kazi wanazozifanya zinatakiwa kuambatana na suala la uzalendo na wasipofanya hivyo hawataweza kupata miradi mbalimbali kutoka serikalini. Anaripoti Danson Kaijage, Kilimanjaro… (endelea)
Wito huo umetolewa leo Jumamosi na Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa wakati akizungumza na wakazi wa Tarakea wilayani Rombo mkoni Kilimanjaro.
Bashungwa amesema Serikali imejipanga kuweka lami barabara ya Holili – Tarakea (km 51), na tayari imeanza na sehemu ya mita 580 na itaendelea kujenga kwa kiwango cha lami km 10 sehemu ambayo haihitaji fidia ili kuharakisha ujenzi wa barabara hiyo.
“Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imedhamiria kuwapa miradi mingi na mikubwa wakandarasi wazawa ili kuwajengea uwezo wa kitaalam na kiuchumi, hivyo kuweni wazalendo na kamilisheni miradi kwa wakati na ubora,” amesema.
Aidha, amemtaka Mkandarasi wa ndani M/s JP TRADERS LTD kuhakikisha anakamilisha ujenzi wa sehemu ya barabara hiyo ifikapo Februari mwakani kulingana na mkataba.
“Rais Samia tayari ameshatoa kibali cha kuongeza kilometa 10 za barabara kwenye ujenzi wa mita 580 unaoendelea katika eneo ambalo halina fidia ili kuongeza kasi ya ujenzi wa barabara hiyo”, amesema.
Aidha, Bashungwa amemtaka Meneja wa TANROADS Mkoa wa Kilimanjaro, Mhandisi Motta Kyando kuhakikisha ujenzi wa barabara hiyo unaenda sambamba na ukarabati wa barabara ya mbadala ili wananchi wasiathirike kutokana na ujenzi huo.
Bashungwa amewahakishia wakazi wa Tarakea wilayani Rombo kwamba tayari usanifu wa barabara ya Elerai – Kamwanga (km 39), umekamilika na ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami utaanza hivi karibuni ili kuboresha shughuli za utalii na kukuza uchumi kwa wananchi.
Leave a comment