MKUU wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Fredrick Shoo, ameomba neno haki, liongezwe katika wimbo wa taifa hilo, kwani ni tunda la amani ya nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro…(endelea).
Askofu Shoo alitoa wito huo jana Jumatatu tarehe 6 Desemba 2021, akifungua semina ya kuwajengea uwezo viongozi wa dini, katika ulinzi na utetezi wa haki za binadamu, iliyofanyika mkoani Kilimanjaro.
Semina hiyo iliandaliwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), kwa kushirikiana na Kamati ya Viongozi wa Dini inayohusu Haki za Kijamii na Uadilifu wa Uumbaji (ISCEJIC).
Huku akiuimba wimbo huo, Askofu Shoo alishauri katika mstari unaopatikana kwenye ubeti wa kwanza wa ‘Mungu ibariki Tanzania, dumisha uhuru na umoja’, liongezwe neno haki.
“Haki ni jambo la msingi, wanasema pasipo haki hakuna amani. Amani ni tunda la haki, sijui lakini nina ndoto na hivi nimeanza sijui kama navunja sheria, tunavyoimba wimbo wa taifa mimi siku hizi kimya kimya nasema dumisha uhuru haki na umoja,” alisema Askofu Shoo.
Kiongozi huyo wa kidini ameshauri mstari huo uimbwe ‘Mungu ibariki Tanzania, dumisha uhuru, haki na umoja’, kwani ni dua inayopelekwa kwa Mungu.
“Naamini kuna wakati itafika itakubalika, Mungu ibariki Tanzania, dumisha uhuru, haki na umoja, wake kwa waume na watoto. Mungu ibariki Tanzania. Unajua ule wimbo ni dua tunapeleka dua zetu kwa njia hii kama taifa,” alisema Askofu Shoo.
Aidha, Askofu Shoo aliwaomba viongozi wa dini wawe mstari wa mbele katika kushiriki kwenye masuala ya kidemokrasia, siasa na kijamii kwani ushiriki wao unaleta tija kwenye uongozi na utawala ndani ya jamii.
“Majukumu ya viongozi kutambua ushiriki katika masuala ya kidemokrasia na siasi, haki ya kijamii na watu wake. Ushiriki wenye tija kwenye masuala hayo ni chanzo cha kupata na kuboresha uongozi na utawala katika jamii na nchi,” alisema Askofu Shoo.
Vilevile, Askofu Shoo aliwashauri viongozi wa dini kushiriki katika majadiliano na utengenezaji wa sera na sheria bora kwa ajili ya maendeleo ya watu na nchi kwa ujumla.
“Viongozi wa dini tunapaswa kuwa na maarifa na uweledi ili kuzilinda na kuzitetea haki za msingi za watu na jamii wanayoishi na kuwaongoza kama viongozi wao wa kiroho, bila kufanya hivyo haki za msingi za watu zitakuwa zinavunjwa kwa kuwa hakuna wa kuwatetea na kuwasemea,” alisema Askofu Shoo.
Leave a comment