KANISA la Gospel Christ Church Tanzania (GCC) limetoa wito kwa jamii kuwajengea watoto misingi ya elimu na hofu ya Mungu ili kuwaandaa kuwa viongozi waadilifu wenye hofu ya Mungu na kupata Taifa lenye mafanikio ya kimaendeleo katika sekta mbalimbali. Anaripoti Danson Kaijage, Nairobi (endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumanne na Mkuu wa Kanisa hilo Askofu Dk. Daud Chidawali wakati akizungumza na waandishi wa habari, baada ya kutunukiwa Shahada ya Uzamivu ya masuala ya dini.
Shahada hiyo ametunukiwa na Chuo cha International Christian University of Ministry Education – Miissouri – USA tawi la Mombasa nchini Kenya.
Amesema bila ya viongozi bora hakuna maendeleo ya kimsingi kama vile ya kiroho, kielimu, kiuchumi, kiafya, kilimo na kijamii hivyo Taifa ni lazima wapatikane wenye kujali mahitaji ya watu ambayo ni ya msingi kwa wanadamu wake.
Dk. Chidawali amesema viongozi hao wanawajibu wa kutambua changamoto zinazowakabili wananchi wao juu ya maisha wanayoishi siku zote ikiwa ni haki yao ya msingi kama vile amani, ardhi, elimu, afya, malazi na chakula.
Hata hivyo, amesema ili Taifa liendelea linahitajika watu wasomi hivyo ninawaomba viongozi wa kidini na kiserikali kuhakikisha wanawaandaa vijana kielimu, ili nchi ipate viongozi watakaopewa dhamana ya kuongoza katika sekta mbalimbali.
“Hivyo niwaombe viongozi wawe wa kidini au kiserikali ni wajibu wetu kuhakikisha suala la elimu tunaliweka kipaumbele kwa watoto wetu kwa ajili ya kuwaanda ili waweze kushika nafasi katika sekta mbalimbali za uongozi,” amesema.
Amesema kuwa wakiandaliwa kwa kusomeshwa Taifa litaepukana na changamoto ya kuwapata viongozi wabovu wanaojijali wao wenyewe badala ya watu wote, pia wasiokuwa na maadili ya kiroho wapenda rushwa na wasiompenda Mungu kwa kuwa walio wengi watakuwa na tabia ya vitendo viovu.
Leave a comment