AGIZO la Rais Samia Suluhu Hassan alilolitoa jana kwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwamba kijana mvuvi- Majaliwa Jackson apatiwe nafasi mafunzo kwenye Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, limetekelezwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Bukoba … (endelea).
Kijana huyo alijitosa katika Ziwa Victoria na kufanikiwa kuokoa watu 24 waliokuwa kwenye ajali ya ndege ya Precision Air iliyoanguka asubuhi tarehe 6 Novemba, 2022 wilayani Bukoba mkoani Kagera.
Licha ya watu 24 kuokolewa wakiwa hai katika ajali hiyo, jumla ya watu 19 walipoteza maisha akiwa rubani wa ndege hiyo na msaidizi wake.
Aidha, taarifa iliyotolewa kwa Umma na Msemaji wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, SACF Puyo Nzalayaimisi imeema Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Kamishna John Masunga kijana huyo anatarajiwa kuanza mafunzi ya zimamoto na uokoaji pamoja na ya uaskari katika Chuo cha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kilichopo Chogo wilayani Handeni mkoani Tanga.
“Majaliwa alionesha ujasiri wa hali ya juu kwa kuokoa wahanga 24 wa tukio hilo,” imesema.
Aidha, imesema Kamishna Jenerali anatoa shukrani za dhati kwa vyombo vya ulinzi na usalama, taasisi za umma, binafsi pamoja na wananchi wa mkoa wa Kagera kwa ushirikiano mkubwa walioutoa katika zoezi la uokoaji katika ajali hiyo.
Pia anatoa pole kwa wafiwa wote na kuwaombea faraja katika kipindi hiki kigumu wanachopitia na anawatakia majeruhi wote afya njema.
“Anawasihi wananchi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji katika kuokoa maisha ya watu na mali dhidi ya majanga mbalimbali,” imesema taarifa hiyo.
Leave a comment