CHAMA cha ACT Wazalendo, kimeitaka Serikali kupitia Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali kufanya ukaguzi maalumu wa matumizi ya fedha za tozo ya miamala ya simu zilizoanza kukusanywa mwaka 2021/22. Anaripoti Apaikunda Mosha, TUDARco…(endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari makao makuu ya chama leo Jumatatu tarehe 12, Septemba, 2022, Msemaji wa Sekta ya Fedha na Uchumi wa chama hicho, Emmanuel Mvula, amesema ukaguzi huo ni muhimu kutokana na mkanganyiko wa kuhusu matumizi ya fedha zilizopaswa za miamala ya simu na zile za mkopo wa UVIKO-19 kutoka IMF.
“Mwaka 2021 Serikali ilitueleza kwamba fedha za mkpo wa UVIKO-19, zilitumika kujenga madarasa shule mpya, vituo vya afya na kuimarisha miundombinu. Serikali inaacha maswali mengi inapojitikeza tena na kueleza fedha za miamala ndiyo zimetumika kwa malengo yaleyale,” amesema Mvula.
Aidha chama hicho kimeitaka Serikali kusitisha tozo hizo kwani zimeendelea kuleta maumivu kwa wananchi huku kukiwa na utozaji mara mbili tangu kuanza kwa tozo za miamala ya benki.
Hata hivyo tayari Serikali kupitia Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba, imesema itaifanyia kazi changamoto hiyo ya mwananchi kukatwa mara mbili.
Lakini Mvula ameendelea kueleza kuwa Serikali imeshindwa kuweka wazi tatizo hilo ni lini litatatuliwa na kwamba Serikali anapuuza malalamiko ya wananchi.
Aidha amesema madhara yanayotokana na tozo ni makubwa kuliko malengo ya kifedha yanayotarajiwa kuvunwa na Serikali.
“Serikali iwafute machozi wananchi kwa kusitisha kabisa tozo hizi na pengo lake lifidiwe kwenye vyanzo vingine ambavyo havitaleta madhara,” amesema Mvula.
Leave a comment