Alisema, “kuna habari nyingi za upotoshaji kuhusu ardhi na wakazi wa Loliondo. Hakuna mtu atakayetolewa kwenye eneo hilo kwa nguvu. Na wala serikali haina mpango wa kuwaondoa au hata kutumia nguvu yoyote dhidi ya wakazi wa maeneo hayo.”
Waziri Ndumbaro, alikuwa akijibu madai yaliyotolewa na Shirika la kutetea haki za Binadamu la Amnesty International, kwamba mamlaka nchini Tanzania zimekuwa zikiwaondoa kwa nguvu watu wa jamii ya maasai kutoka katika eneo la Loliondo.
Shirika hilo limesema, Juni 2022, vikosi vya ulinzi na usalama vilitumia nguvu kupita kiasi, kuwakamata watu kiholela na kuwafyatulia risasi katika eneo Loliondo, lililopo katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
Shirika la kutetea haki za Binadamu la Amnesty International limelaani mamlaka nchini Tanzania kwa kudai kuwaondoa kwa nguvu watu wa jamii ya maasai kutoka katika eneo la Loliondo.
Waziri Dk. Ndumbaro ameliambia shirika la habari la Uingereza (BBC), kwamba kilichofanyika mwaka jana katika eneo la pori tengefu la Loliondo, ni zoezi wa uwekaji alama za ardhi na kwamba hakuna mtu aliyehamishwa.
Dk. Ndumbaro alisema kuwa wakati wa zoezi hilo, wananchi waliokuwa na silaha za jadi waliingia kuwavamia polisi ambao walikuwa na silaha za moto lakini walizingatia weledi.
“Polisi wetu walifanya kazi kwa weledi sana katika zoezi la uwekaji, hata baada ya kuvamiwa na wananchi waliokuwa na mapanga hawakujibu kwa kupiga risasi kwa sababu, waliheshimu haki za binadamu na hata baada ya kufanya hivyo, askari mmoja aliuwawa,” alieleza.
Kwa mujibu wa serikali, eneo la kilometa za mraba 4,000 (elfu nne), Loliondo lilikuwa eneo kwa ajili ya uhifadhi na lilianzishwa na serikali ya kikoloni ya Ujerumani; badaye likatambuliwa na serikali ya Uingereza na baada ya uhuru lilikuwa katika hali ya uhifadhi.
Dk. Ndumbaro anasema, baada ya uhuru wananchi walivamia eneo kubwa na kusababisha kutoweza kutumika kwa ajili ya uhifadhi na hivyo serikali ikaamua kilomita za mraba 2,500 ambayo ni asilimia 67.5 ya eneo lote la Loliondo, wakabidhiwe wananchi kisha kubaki na kilomita za mraba 1500 za eneo tengefu.
Mashauri yaliofanywa Septemba mwaka jana, Mahakama ya Afrika Mashariki (EACJ), ilitupilia mbali ombi la baadhi ya wanajamii ya kimaasai katika kesi iliyohusisha mgogoro wa ardhi kati yao na serikali ya Tanzania.
Wananchi hao walitaka Mahakama hiyo ya kikanda kuizuia Serikali ya Tanzania kuwaondoa kwa nguvu katika eneo hilo.
Leave a comment