Saturday , 27 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Bunge labaini madudu mfumo ukusanyaji mapato, h’shauri tatu kikaangoni
Habari za Siasa

Bunge labaini madudu mfumo ukusanyaji mapato, h’shauri tatu kikaangoni

Mwenyekiti wa LAAC, Stanslaus Mabula
Spread the love

 

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), imedai kuwa, kuna changamoto ya uvujaji wa mapato ya Serikali katika mfumo wa kielektroniki wa kukusanya mapato, inayotokana na baadhi ya watumishi kuuchezea mfumo huo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).

Hayo yamebainishwa leo tarehe 7 Februari 2023, bungeni jijini Dodoma na Mwenyekiti wa LAAC, Stanslaus Mabula, akiwasilisha taarifa ya shughuli za kamati hiyo kwa mwaka 2022.

“Kamati ina maoni kwamba kinachofanyika ni wizi kwa sababu ya mazingira ambamo marekebisho ya miamala hufanyika. Kuna maeneo ambamo miamala hufutwa kabisa au baadhi ya tarakimu hurekebishwa bila idhini ya Maafisa Masuuli au bila ya kuwepo kwa nyaraka za uthibitisho wa uhalali wa marekebisho hayo,”amesema Mabula.

Mabula ametaja baadhi ya halmashauri zinazokabiliwa na changamoto hiyo, ikiwemo Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo, ambayo inadaiwa kuwa mfumo wake wa ukusanyaji mapato ulichezewa.

Hali hiyo ilisababisha kushindwa kuonesha mapato yake halisi kwa kuingiza kiasi cha Sh. 500,666,683,784,266,000,000,000, kisha baadae kufutwa kwa maelezo kwamba kilikosewa. Hata hivyo, manispaa hiyo inadaiwa kutotoa maelezo ya kiasi halisi kilichotakiwa kuandikwa kilikuwa kipi.

Akiendelea kusoma taarifa hiyo, Mabula amesema mnamo tarehe 16 Juni 2019, muamala wa Sh. 471.4 milioni ulirekebishwa katika mfumo huo na Sh. 450 milioni, bila idhini ya afisa masuuli. Marekebisho hayo yanadaiwa kuleta upungufu wa Sh. 21.3 milioni, ambazo zinadaiwa kuchukuliwa na watumishi waliohusika na marekebisho hayo.

Manispaa nyingine iliyokabiliwa na changamoto hiyo kwa mujibu wa LAAC, ni ya Kigamboni, ambapo baadhi ya watumishi wake walifanya marekebisho ya miamala ya mapato ya kiasi cha Sh. 10.8 milioni bila idhini ya afisa masuuli.

Mabula ametaja manispaa nyingine kuwa ni ya Ilemela, jijini Mwanza, ambapo anadai kwamba ankara zenye thamani ya Sh. 8.7 bilioni zilirekebishwa kwenye mfumo wa mapato bila kufuata utaratibu.

Wakati kiasi cha Sh. 627.8 milioni, hazikuepelekwa benki, huku kukiwa hakuna ushahidi wa malipo ya kiasi cha Sh. 356.4 milioni, kwamba zililipwa kwa mhandisi mshauri elekezi katika usimamizi wa mradi wa stendi ya mabasi na maegesho ya malori.

“Manispaa ilimlipa Mkandarasi (TBA) kiasi cha Sh. 138.7 milioni kwa kazi ambazo hajafanya, watumishi waliohama na wengine kustaafu wakawa bado wanaingia kwenye mfumo wa mapato kiasi cha kutishia usalama wa mfumo wa Serikali katika ukusanyaji wa mapato na katika hesabu za mwisho kwa mwaka wa fedha 2019/20 Manispaa iliripoti zaidi,” amesema Mabula.

Kutokana na changamoto hizo, Mabula amesema, “maoni ya Kamati ni kwamba Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela inapaswa kufuatiliwa kwa karibu kuhusiana na mwenendo wake katika kukusanya na kutumia mapato yake. Ofisi ya RaisTAMISEMI inatakiwa kuisimamia kikamilifu Manispaa hii na kuchukua hatua kali dhidi ya watumishi ambao utendaji wao ulisababisha kuwepo kwa hoja hizo.”

Mabula amesema LAAC inaishauri Serikali kudhibiti mianya ya uvujaji wa mapato katika mfumo mpya wa TAUSI, kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika mifumo ya ukusanyaji mapato kwa njia za kielektroniki ili kujiridhisha dhidi ya ufanisi wake, pamoja na kuwachukulia hatua za kisheria waliohusika na uvujaji huo.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Sauti ya Watanzania waeleza sababu za kuiunga mkono Chadema

Spread the love  KIKUNDI kinachojipambanua katika kupigania rasilimali na uhuru wa nchi,...

Habari za SiasaKimataifaTangulizi

Tanzania, Somalia kuibua maeneo mapya ya ushirikiano

Spread the love  RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema Tanzania na Somalia...

Habari za Siasa

ACT: Waongoza watalii wapate maslahi yao inavyostahili

Spread the loveCHAMA cha ACT-Wazalendo kimeitaka serikali kuhakikisha inasimamia maslahi stahiki ya...

Habari za SiasaTangulizi

Prof. Lipumba ajitosa kuviunganisha vyama vya siasa Burundi

Spread the love  MWENYEKITI wa Kituo Cha Demokrasia Tanzania (TCD), Prof. Ibrahim...

error: Content is protected !!