BODI ya Maji ya Bonde la Wami Ruvu imesema kuwa imejipanga kuhakikisha inamaliza changamoto ya tatizo la maji katika mikoa ya Dar es salaam,Pwani na Morogoro kwa kuchimba visima kumi vyenye maji ya kutosha. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Hayo yamebainishwa leo Tarehe 7 Februari 2023 na Mkurugenzi wa Bodi ya Maji Bonde la Wami Ruvu, Mhandisi Eribariki Mmasi, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa habari maelezo Jijini Dodoma juu ya utekelezaji wa miradi ya maji chini ya bodi hiyo.
Mhandisi Mmasi amesema kuwa bodi hiyo imejipanga kuhakikisha inatatua tatizo la maji katika mikoa ambayo imekuwa na changamoto ya maji hususani katika mkoa wa Pwani, Morogoro na Dar es salaam.
Hata hivyo Mhandisi Mmasi amesema kuwa Bodi hiyo imeweza kutekeleza miradi ya maji katika mikoa sita ambayo ameitaja kuwa ni Morogoro, Dar es Salaam, Pwani, Dodoma, Tanga, Manyara pamoja na wilaya 27.
Amesema kuwa nia ya kuanzishwa kwa bodi ya maji ni pamoja na kuhakikisha rasilimali za maji zinalindwa,kutunzwa na kuendelezwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kizazi kijacho sambamba na kuhakikisha utunzaji wa mazingira unatekelezwa.
Pamoja na mambo mengine Mhandisi Mmasi amesema kuwa Bodi ya maji imeweza kufanikiwa kubaini vyanzo vipya vya maji ambavyo amevitaja kuwa ni eneo la Nzuguni lililopo Jijini Dodoma kuwa lina maji ya kutosha na hivi karibuni litatangazwa katika gazeti la serikali kuwa ni benki ya maji pamoja na Dakawa katika mji wa Dodoma.
Kuhusu utunzaji wa vyanzo vya maji Mhandisi Mmasi amesema kuwa wanahakikisha vyanzo vyote vinatunzwa kwa ajili ya kutunza maji yaliyopo chini ya ardhi huku akiwataka watanzania kuepukana na tabia ya uchimbaji hovyo wa visima vya maji kwa maelezo kuwa kunaweza kusababisha kuchafua maji yaliyopo chini ya ardhi jambo ambalo ni hatari.
Leave a comment