SERIKALI ya Tanzania iko mbioni kuifanyia marekebisho Sera ya Habari na Utangazaji ya 2003 ili iendane na wakati pamoja na kuondoa mapungufu yake. Anaripoti Regina Mkonde,Dar es Salaam…(endelea).
Hayo yamesemwa leo Jumamosi na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile, akizungumza na MwanaHALISI Online kuhusu maendeleo ya mchakato wa marekebisho ya Sheria za habari Tanzania.
“Hizi sheria nyingine bado sababu tulitaka tupambane na ajenda moja hiyo Sheria ya Huduma za Habari ishakwenda hizi nyingine Waziri wa Habari amekuja na wazo ya kwamba tukishamaliza Sheria ya habari tuanze mchakato wa mabadiliko ya sera ya habari maana sera tuliyonayo ni ya 2003,” amesema Balile.
Balile amesema baada ya sera hiyo kurekebishwa, Serikali na wadau wataangalia namna ya kuwa na sheria moja ya vyombo vya habari, badala ya kuwa na sheria nyingi zinazosimamia tasnia hiyo.
Mbali na sera hiyo kupitwa na wakati, Balile ametaja mapungufu yake mengine ikiwemo kutoruhusu raia wa kigeni kumiliki vyombo vya habari.
“Sera hii ikiboreshwa tutaweza kuwabana watu wa matangazo lazima walipe vyombo vya habari tofauti na sasa hivi wanaweza wasilipe na hawachukuliwi hatua yeyote. Sera inatoa mwanya kwa Serikaki isitoe matangazo kwa vyombo vya habari binafsi,” amesema Balile.
Naye Mjumbe wa Kamati Tendaji ya TEF, Nevil Meena, amesema Sera hiyo ikifanyiwa Marekebisho itaenda sambamba na marekebisho yatakayofanywa katika Sheria zinazosimamia tasnia ya habari.
“Sera huwa inatangulia, Sheria inafuata. Kimsingi mabadiliko yanayofanywa kwenye Sheria lazima yaathiri sera sababu Sheria haiwezi kukiuka katiba na sera,” amesema Meena na kuongeza:
“Lakini pia kama Kuna mahali marekebisho yamefanywa kwenye Sheria na yakakinzana na sera lazima sera ibadilike Ili iweze kuendana.”
Taarifa hiyo imekuja baada ya Serikali kutangaza Nia ya kuwasilisha bungeni Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Huduma za Habari ya 2016, Ili kuondoa vifungu vinavyolalamikiwa na wadau kwamba vinakandamiza uhuru wa habari.
Leave a comment