WAZIRI wa Fedha na Mipango Tanzania, Dk. Mwigulu Nchemba amependekeza, kupunguza tozo kwa makosa yanayofanywa barabarani na pikipiki maarufu ‘bodaboda na Bajaji itakuwa Sh.10,000 kutoka Sh.30,000 kwa kosa moja. Anaripoti Jemima Samwel, DMC…(endelea).
Akiwasilisha Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2021/22, bungeni jijini Dodoma, leo Alhamisi, tarehe 10 Juni 2021, Dk. Mwigulu amesema “lengo la hatua hii ni kuweka adhabu kwa kuzingatia uwezo wa kulipa.”
“Aidha, adhabu kwa makosa mengine ya vyombo vya moto zinazotolewa kwa mujibu wa Sheria zinaendelea kubaki kama ilivyo sasa.”
Amesema, vijana wengi wamejiajiri kwenye sekta ndogo ya kuendesha bajaji na pikipiki zikijulikana kama bodaboda.
Waziri huyo amesema, hata hivyo, vijana hawa hupata usumbufu mkubwa wa kulipa faini kutoka kwenye vipato vyao pale panapotokea uvunjaji wa Sheria ya Usalama Barabarani umefanywa na abiria wao.
“Hali hii imekuwa ikisababisha baadhi yao kushindwa kulipa faini na hivyo kuzitelekeza pikipiki zao kwenye vituo vya polisi. Mheshimiwa Rais (Samia Suluhu Hassan) alielekeza jeshi la Polisi kujikita kwenye kutoa elimu kuhusu usalama barabarani badala ya kuwekeza kwenye makosa na kugeuza faini kuwa chanzo cha mapato,” amesema
Leave a comment