SERIKALI ya Tanzania, imepanga kutoa msamaha wa kodi ya ongezeko la thamani (VAT), kwenye simu janja za mkononi, vishikwambi (Tablets) na modemu, ili kuhamasisha matumizi ya huduma za mawasiliano. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Alhamisi, tarehe 10 Juni 2021 na waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba, akiwasilisha Bajeti Kuu ya Serikali kwa 2021/22, bungeni jijini Dodoma.
Dk. Mwigulu amesema, hatua hiyo imechukuliwa ili kufikia lengo la asilimia 80, ya watumiaji wa intaneti ifikapo 2025, kutoka asilimia 46 iliyopo.
“ Sekta ya mawasiliano imekuwa ikikua vizuri na kuwa kiungo muhimu cha kuongeza wigo wa wananchi, ambao wako kwenye ulimwengu wa kidijitali na kwenye sekta ya fedha (Financial Inclusion). Napendekeza kusamehe VAT, kwenye simu janja za mkononi (smart phones) HS Code 8517.12.00,” amesema Dk. Mwigulu.
Waziri huyo ameongeza “ vishikwambi (Tablets) HS Code 8471.30.00 au 8517.12.00 na modemu (modems) HS Code 8517.62.00 au 8517.69.00. Lengo la hatua hii ni kuhamasisha matumizi ya huduma za mawasiliano, ili kufikia lengo la asilimia 80 ya watumiaji wa intaneti ifikapo mwaka 2025.”
Leave a comment