SERIKALI ya Tanzania, inatarajia kuanzisha utaratibu mpya wa usimamizi wa fedha na matumizi ya taasisi zianzotoza ada, katika mwaka wa fedha wa 2021/22. Anaripoti Jemima Samwel, DMC…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Alhamisi, tarehe 10 Juni 2021 na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba, akiwasilisha mapendekezo ya Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha wa 2021/22, bungeni jijini Dodoma.
Dk. Mwigulu amezitaja taasisi hizo kuwa ni, Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na Wakala wa Meli Tanzania (TASAC).
Akielelezea utaratibu huo, Dk. Mwigulu amesema kuanzia Julai 2021, mapato yanayokusanywa na taasisi hizo , yatapelekwa kwenye akaunti za makusanyo, zilizopo Benki Kuu.
“Ili kuendelea kuimarisha usimamizi wa fedha za umma kwa taasisi zinazotoza ada, Serikali inaweka utaratibu mpya na endelevu wa kusimamia mapato na matumizi ya TPA, TCRA na TASAC.
Hivyo, kuanzia mwaka 2021/22, mapato yataendelea kukusanywa na taasisi hizo kupitia mfumo wa GePG na kuingizwa kwenye akaunti za makusanyo (holding account) zilizopo Benki Kuu,” amesema Dk. Mwigulu.
Waziri huyo wa fedha amesema, taasisi hizo zitapatiwa fedha kulingana na bajeti inayoidhinishwa, kwa idhini ya mlipaji mkuu wa Serikali.
“Aidha, taasisi hizi zitapatiwa fedha kulingana na bajeti iliyoidhinishwa na fedha kutolewa kwenye akaunti ya makusanyo, baada ya kupata ridhaa ya mlipaji mkuu wa Serikali. Vilevile, Serikali itafanya ufuatiliaji wa matumizi ya taasisi hizi kila robo mwaka,” amesema Dk. Mwigulu.
Leave a comment