ABOUBAKAR Kunenge, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam amstukiza mkandarasi wa ujenzi wa Soko la Tandale ili kujiridhisha kama ametekeleza maagizo ya kufanya kazi kwa saa 24 za siku. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Mkuu huyo wa mkoa amefanya ziara hiyo ya kushtukiza usiku wa manane kuamkia leo tarehe 22 Desemba 2020, baada ya siku mbili kupita tangu alipotoa agizo kwa mkandarasi huyo kufunga taa za usiku ili afanye kazi muda wote.
Agizo la kumtaka mkandarasi huyo kufanya kazi muda wote alilitoa kwenye ziara aliyoifanya Jumamosi tarehe 19 Desemba 2020 ambapo pamoja na kufanya kazi kwa saa 24, alimtaka kuongeza idadi ya vibarua ili amalize kwa muda uliopangwa.
Baada ya ziara hiyo, Kunenge amesema, mkandarasi huyo wa Kampuni ya NAMIS CORPORATE ametekeleza maagizo kwa kufunga taa na kuongeza vibarua ili ujenzi huo uweze kukamilika kabla ya Aprili mwakani.
Aidha Kunenge ametuma salamu kwa wakandarasi wote wanaotekeleza miradi Jijini humo kuzingatia mikataba yao kwa kuhakikisha wanakamilisha miradi kwa wakati ili iweze kutatua kero za wananchi kama serikali ilivyokusudia.
Leave a comment